Na Joyce Kasiki,Tanga
MWENYEKITI wa Bodi ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Profesa John Kondolo, amesema taasisi hiyo inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wabunifu nchini ili kukuza bunifu zao na kuzifikisha katika soko.
Akizungumza na waandiahi wa habari katika banda la Taasisi hiyo ,Profesa Kondolo amesema COSTECH inashiriki katika maonesho na mashindano ya kitaifa ya Elimu,Ujuzi na Ubunifu yanayolenga kuhamasisha ubunifu, huku ikitoa fursa kwa wabunifu kuonesha bidhaa na teknolojia walizozibuni.
Amesema mbali na maonesho ya bunifu, mashindano ya maarifa yanayoandaliwa katika matukio hayo yanasaidia pia kuchochea ubunifu miongoni mwa vijana na jamii kwa ujumla.
“Tunakuwepo ili kuchochea ubunifu mbalimbali, kuwezesha ubunifu huo kukua na kuwasaidia wabunifu,” amesema Profesa Kondolo.
Kwa mujibu wa Profesa Kondolo, COSTECH iko tayari kusaidia wabunifu kifedha na kuwezesha bunifu zao kufikia hatua ya kuingia katika soko, badala ya kubaki katika hatua ya mawazo au majaribio.
Amesema COSTECH inashirikiana na taasisi mbalimbali za elimu na mafunzo ya ufundi, ikiwamo Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), pamoja na taasisi za elimu ya juu kama Chuo cha Taifa cha Usafirishaji na Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) na Arusha Technical College.
Profesa Kondolo amewataka wabunifu kutumia fursa zinazotolewa na taasisi hizo ili kuboresha uwezo na ubunifu wao, hatua ambayo itawawezesha kuandaa bidhaa zenye ubora na ushindani katika soko.
Amesema ushirikiano kati ya COSTECH, taasisi za elimu na wadau wengine ni muhimu katika kujenga mfumo utakaowawezesha wabunifu kutoka kwenye wazo, kutengeneza bidhaa na hatimaye kufikia soko.

More Stories
VETA yatengeneza Simu yake ya kwanza
Serikali:Elimu ya ujuzi yaanza kuzaa matunda
ITA Yatumia Maonesho Kuhamasisha Vijana Kusoma Kodi