August 18, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkenda: Tanzania yawekeza katika Sayansi, Ubunifu kujenga Taifa

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Tanga

SERIKALI imeendelea kuongeza uwekezaji katika elimu, ujuzi, sayansi, teknolojia na ubunifu kwa lengo la kujenga uwezo wa Watanzania kutengeneza teknolojia na suluhisho za ndani zitakazopunguza utegemezi wa wataalamu na teknolojia kutoka nje.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema hayo Agosti 18, 2026 jijini Tanga wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026.


Profesa Mkenda amesema Tanzania ina wataalamu wenye uwezo mkubwa, lakini wanahitaji mazingira bora na fursa za kutumia maarifa yao katika kubuni bidhaa na huduma zitakazosaidia kutatua changamoto za wananchi na kuchochea maendeleo ya Taifa.


Amesema utafiti na ubunifu vinapaswa kuelekezwa katika maeneo yenye changamoto kubwa kwa jamii, yakiwemo kilimo, afya, uzalishaji na mazingira, huku teknolojia zinazobuniwa zikizingatia matumizi endelevu ya rasilimali na mahitaji ya kizazi cha sasa na kijacho.


“Serikali inatoa ufadhili wa asilimia 100 kwa lengo la kujenga sayansi na teknolojia nchini,” amesema.


Kwa mujibu wa Waziri huyo, Serikali imeendelea kujenga shule za sayansi katika mikoa mbalimbali na kutoa ufadhili wa elimu ya juu kwa wanafunzi wenye vipaji, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wataalamu katika sayansi na teknolojia.


Pia amesema maboresho ya sera na mitaala ya elimu yanaendelea kufanyika ili kuifanya sekta hiyo kuwa kichocheo cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, pamoja na kuwaandaa vijana kukabiliana na mahitaji ya dunia inayobadilika kwa kasi kiteknolojia.


Profesa Mkenda ameeleza kuwa vijana wanaofanya vizuri katika ubunifu wameanza kupata fursa za kushiriki mashindano ya kimataifa, jambo litakalosaidia kupima uwezo wa Tanzania katika teknolojia na ubunifu dhidi ya mataifa mengine.


Amewataka taasisi za elimu, watafiti, wabunifu, vijana na wadau mbalimbali kushirikiana na Serikali katika kutumia elimu, ujuzi, sayansi na teknolojia kujenga Tanzania yenye uwezo wa kuzalisha wataalamu, bidhaa na teknolojia zenye ushindani ndani na nje ya nchi.


Katika uzinduzi huo uliofanyika katika viwanja vya Usagara jijini Tanga, Waziri Mkenda pia alikabidhi tuzo kwa watafiti 154 waliobobea katika tafiti zilizochapishwa kwenye majarida ya kimataifa. Washindi hao walitoka katika nyanja za sayansi asilia, afya na sayansi shirikishi, kilimo na wanyama, pamoja na uhandisi na TEHAMA, huku wakipatiwa vyeti na zawadi za fedha zenye jumla ya Sh milioni 50.