May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Chagulani kuanza na afya, elimu, biashara

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

MGOMBEA Ubunge Jimbo la Nyamagana kupitia Chama cha ACT-Wazalendo, Adam Chagulani ameeleza vipaumbele vyake endapo atapata ridhaa ya kuwa Mbunge wa Jimbo hilo ni pamoja na afya, elimu, biashara, maji na miundombinu mbalimbali.

Chagulani ameuambia Mtandao huu kuwa, atahakikisha anaboresha huduma za afya na vituo vya afya ili viwe na vifaa tiba kwani jimbo hilo lina Kata 18 ambapo baadhi yao hazina zahanati ikiwemo ya Kata ya Luchelele wakati muongozo wa Wizara ya Afya unaelekeza kila Kata iwe na kituo cha afya.

Lakini pia atasimamia suala la watumishi wa afya kuajiriwa, kufuata muongozo wa daktari mmoja ahudumie watu 1000 kwani sasa daktari mmoja anahudumia watu 30,000.

Lengo la kuboresha vituo vya afya ni pamoja na huduma za afya ya mama na mtoto ili kuwe na mazingira mazuri yatakayomfanya mama na mwenzi wake waweze kupata elimu ambayo itamsaidia kuelewa namna gani ya kuhudumia wakati wa ujauzito na hatua zipi wachukue wakati wa kujifungua pamoja na kupatikana vifaa tiba na madawa ili kuokoa maisha ya mama na mtoto pamoja na huduma ya mtoto na wazee.

Kipaumbele kingine ni kuboresha sekta ya elimu ambapo atahakikisha madasara yanajengwa ili kuondoa mrundikano wa watoto darasani ambao unapelekea mwalimu kushindwa kubaini wale ambao hawaelewi pia kusimamia wanafunzi wanaosoma shule binafsi kupata mikopo wafikapo vyuo vikuu.

Pia ataboresha mazingira ya kufanyia biashara ya wafanyabiashara ndogo ndogo na kujenga masoko ya kudumu na ya kisasa ili kuondoa msongamano na ndani yake na watasajili ushirika wa wafanyabiashara ambapo kupitia ushuru Halmashauri itachukua asilimia 70 na 30 itabaki kwa wafanyabiashara kwa ajili ya kuboresha zaidi masoko na kuwaanzishia Saccos kwa ajili ya kukopeshana wenyewe huku bodaboda wakitengenezewa stendi za kisasa kama ilivyo za daladala.

Amesema kuwa, pia atasimamia kupatikana maji ya uhakika kwa Jimbo hilo zima kwa kuwa na mpango kabambe hivyo kazi hiyo ataifanya na kuweza kuyasemea hayo yote endapo watampatia ridhaa hiyo kwa kushirikiana na kuishauri Serikali.