April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM yashusha maelekezo kwa Bandari ya mtwara,Wizara ya afya

Na Mwandishi wetu,timesmajira,Online

KATIBU wa Halmashuri Kuu ya CCM Taifa Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka ametoa maagizo kwa Uongozi wa Bandari ya Mtwara ikiwemo kuhakikisha bandari hiyo kuanza kutoa huduma za haraka ili kuzalisha ajira, kuchochea uchumi wa Mtwara na nchi pia.

Pia ameitaka mamlaka hiyo ya bandari kuweka mkakati thabiti wa kuitangaza bandari hiyo ili wafanyabiashara na wawekezaji mbalimbali waijue na waitumie kuingiza na kusafirisha mizigo yao.

Akitoa maagizo hayo leo, Septemba17 2021, akiwa Wilayani Mtwara ikiwa ni muendelezo wa ziara ya wajumbe na sekretariet inayoongozwa na Katibu Mkuu Daniel Chongolo.

Amesema pamoja na uwekezaji Mkubwa uliofanyika katika bandari hiyo wa takribani bilioni 158.8 za kuboresha ni ajabu haitoi huduma kama ilivyokusudiwa. “Sababu ikiwa ni urasimu na hata hujuma zinazofanywa na baadhi ya watendaji wa kiserikali kwa kushirikiana na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu,” amesema Shaka

Amesema Chama chao hakitakubali kuona utekelezaji wa ilani yao ya uchaguzi unakwamishwa kwani kufanya hivyo ni kumkwamisha Rais Samia Suluhu Hassan na kuchelewesha maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

“Haiwezekani Rais Samia amemtuma Waziri Mkuu Majaliwa lakini baadhi ya watendaji wasiwaminifu wamepuuza maagizo hayo kamwe CCM haitamvumilia yoyote mwenye nia ovu ya kukwamisha jitihada za Rais Samia katika kuwaletea maendeleo watanzania atakwama yeye,”amesema Shaka Mwenezi Taifa

Wakati huo huo Shaka ameitaka Wizara ya Afya kuacha sinema za maonesho kwa kutoa maelekezo na ahadi zisizotoa matokeo yanayopimika na kuonekana kwa wananchi.

“Naitaka wizara ya Afya kueleza kama walimdanganya Makamu wa Rais wa Tanzania Dkt Philip Mpango alipofika kuweka jiwe la msingi mapema mwezi Oktoba katika Ujenzi wa hospital ya kanda Mtwara inayogharimu takribani bilioni 15, ambapo walimwambia kuwa itakuwa imeanza kutoa huduma lakini ajabu mpaka leo hakuna dalili hizo. “amesema na kuongeza

“Sasa ni vizuri wabadilike waanze kuwa watendaji badala ya kuwa wapiga maneno matupu…pamoja na kasi nzuri ya ujenzi inayofanywa na mkandarasi ambaye ni shirika la Nyumba la Taifa, wizara hiyo imekuwa kikwazo kikubwa katika kuhakikisha hospitali hiyi inakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi,”amesema