May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vijana wakifurahia jambo

Askofu Mafuja awashauri vijana kutotumika kisiasa

Na Judith Ferdinand,TimesMajira,Online Mwanza

VIJANA wametakiwa kujihadhari na waepuka kutumiwa vibaya na baadhi ya wanasiasa au wagombea wa vyama mbalimbali ili kuvuruga amani ya nchi katika kipindi hiki cha kampeni na kuelekea uchaguzi mkuu pamoja na kutangazwa matokeo.

Wito huo umetolewa na Askofu wa Kanisa la Africa Inland Church Tanzania (AICT) Dayosisi ya Mwanza, Philipo Mafuja,wakati akizungumza na timesmajira,Online ofisini kwake mkoani Mwanza.

Amesema duniani kote kundi la vijana ndio uwa linatumiwa vibaya hususani na wanasiasa kufanya fujo hivyo wanapaswa kutambua baada ya uchaguzi kuna maisha yanayoendelea na ni kipindi kifupi tu hivyo wasikubali kutumiwa kuharibu maisha yao.

Askofu Mafuja, amesema tamaa ya kupewa 5,000 au 10,000,kufanya fujo kwa vile mgombea ameona dalili za kushindwa na kutafuta mazingira ya kutaka kuharibu amani siyo jambo zuri, hivyo aliwasihi kuwa siyo vizuri kufanya vitendo kama hivyo kwa sababu inaweza kuleta machafuko wakati nchi ya Tanzania ni kisiwa cha amani.

“Kiukweli tunasikia kwenye vyombo vya habari kiuhalisia vita siyo kitu kizuri hata kidogo,maana yake makundi yanayoumia ni wanawake,watoto,wazee na walemavu ndio wanaoathirika pale inapotokea vurugu kwenye nchi, lakini vijana na wanaume uwa wanakimbia,vijana ndio nguvu kazi katika taifa na jamii kwa hiyo niwasihi vijana mimi kama kiongozi wa dini wajihadhari,wajiepushe na tamaa na wasikubali kutumika,”amesema Askofu Mafuja.

Pia aliendelea kutoa wito kwa wananchi ambao ni wafuasi wa vyama na wagombea wa vyama mbalimbali,ambapo amesema ni vizuri waendelee kutambua kuwa haiwezekani wagombea wote wakashinda nafasi za urais, ubunge na udiwani,lazima apatikane mmoja, hivyo ifikie mahali wawe waungwana wa kukubali matokeo pale wanaposhindwa na kuridhika kwa kura watakazo pata bila kuleta vurugu na kuingiza taifa kwenye machafuko.

Mkutano wa kampeni

Sanjari na hayo alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa viongozi wenzake wa dini kuendelea kutoa elimu kwa vijana waliopo kwenye nyumba za ibada kuwafundisha na kuwahasa ili wajihadhari na vurugu kwani maisha siyo tu wakati wa kampeni.

mkutano wa kampeni

Vilevile amesema,katika kipindi hiki kunaweza kuwa na hofu kwa vyama pinzani kuwa kutakuwa na kura ambazo zinaweza kuibiwa ina weza kuwa ni kutokana na kila chama kinavyo tathimini na kutoa mtazamo wake na hawawezi kuwazuia mtu kutoa mtazamo wake, lakini Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ambayo inasimamia uchaguzi imeahidi kufuata sheria na haki na kutoa nafasi kwa vyama vya siasa kutoa malalamiko.