April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Adakwa na Polisi akituhumiwa kumuingilia kuku hadi kumuua

Na Judith Ferdinand, Timesmajiraonline, Mwanza

POLISI mkoani Mwanza inamshikilia, Rogers Sunday (41) Mkazi wa Usagara wilayani Misungwi kwa tuhuma ya kumuingilia kuku hadi kusababisha kifo chake kwa lengo la kujiridhisha kimwili.

Kutokea kwa tukio hilo kumethibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa, wakati akizungumza na waandishi wa habari jana.

Alisema mtuhumiwa huyo alifanya kitendo hicho Aprili 12, 2024 saa 6 katika kijiji na Kata ya Usagara wilayani humo.

“Tukio hilo limetendeka sebuleni kwenye nyumba ya dada yake mtuhumiwa na kushuhudiwa na mtoto wa kike wa dada yake, ambaye alikuwepo hapo nyumbani, bado tunachunguza chanzo cha tukio hilo pamoja na kuchunguza afya yake ya akili,” alisema Kamanda Mtafungwa.

Habari za kuaminika ambazo gazeti hili limezipata, kuku huyo alikuwa anataga, hatua ambayo ilimuwezesha kijana huyo kumkamata kwa urahisi na kumuingilia, huku hyo huku akilalamika.

Habari hizo zilieleza kwamba baada ya kumaliza haja yake alimtupa kuku huyo nje, huku kuku huyo akiwa tayari amekata roho, kwani inaelezwa alimbana kwa nguvu wakati akielekea kutimiza tamaa zake za mwili.

Katika tukio jingine, Mutafungwa alisema jeshi lao linamshikilia Jackson Kalamaji mkazi wa Wilaya ya Sengerema kwa kosa la kumchoma kisu mke wake, Mariam Bulacha.

Alisema tukio hilo lilitokea Aprili 13 muda wa saa moja usiku. Alisema Kalamaji alimchoma kisu mke wake kwa kumhisi ana mahusiano ya kimapenzi na mwanaume mwingine.