April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kapinga:Kuna mafanikio katika utekelezaji miradi ya kimkakati

Joyce Kasiki,Dodoma

NAIBU Waziri wa Nishati Judith Kapinga ameeleza mafanikio ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta ya Nishati inayojengwa chini ya Serikali ya awamu sita chini ya uongozi wa Rais Dkt.Samia suluhu Hassan.

Kapinga ameyasema hayo wakati akizungumza baada ya kutembelea mabanda ya maonesho bungeni jijini Didoma katika wiki ya Nishati 2024 kujionea   jinsi Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati na Wadau wake walivyojipanga kwa ajili ya kuwahudumia wananchi katika maeneo yao.

“Katika miaka mitatu ya uongozi wa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kazi kubwa imefanyika katika Sekta ya Nishati ..,kwa mfano kuna  utekelezaji wa miradi mbalimbali kama vile  Julius Nyerere (JNHPP) ambao umeshaanza kuzalisha umeme, miradi ya usambazaji umeme mijini, vijijini na vitongojini, nishati safi ya kupikia pamoja na sekta ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia.”amesema Kapinga

Aidha, Kapinga ametumia nafasi hiyo kumshukuru  Spika wa Bunge, Dkt.Tulia Ackson kwa kutoa ushirikiano kwa Wizara ya Nishati ambao umewezesha Wiki ya Nishati kufanyika kwa umahiri mkubwa

 Ametoa wito kwa  Wabunge  kutembelea Maonesho ya Wiki ya Nishati yanayoendelea katika Viwanja vya Bunge jijini Dodoma ili kufahamu masuala mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa miradi mbalimbali chini ya Serikali ya Awamu ya Sita.

“ Katika mabanda haya tasisi zetu zinaonesha namna gani zinatekeleza miradi mbali mbali yenye mabufaa makubwa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla,hivyo niwaombe na niwakaribishe wabunge kwenye Wiki hii muhimu sana ya Nishati, maana hapa tunatatua kero mbalimbali zinazowasilishwa na  Wabunge na Wananchi watajionea utekelezaji wa miradi katika wilaya zote, majimbo yote na mikoa yote Tanzania.”  Ameema Kapinga

Aidha Naibu Waziri huyo amesema,katika Maonesho hayo Taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Nishati pamoja na kampuni zake tanzu zimeshiriki.

Maonesho ya Wiki ya Nishati yameanza April 15 na yanatarajiwa kuhitimishwa April 19 mwaka huu.