May 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Shule za sekondari za ufundi kufufuliwa

Na Joyce Kasiki,Timesmesmajira online,Dodoma

SERIKALI imedhamiria kufufua na kurudisha shule za sekondari za ufundi ambazo zitaanza kuchukua wanafunzi kuanzia Januari mwakani huku shule hizo zikitajwa kuwa ni Iyunga ,Musoma,Ifunda,Tanga,Moshi,Mtwara,Bwiru,Mwadui na Chato.

Mbali na hilo imesema ,imetoa mapendekezo ya namna nzuri ya kuajiri  walimu wa kuanzia elimu ya awali,msingi,sekondari na vyuo vya ualimu hapa nchini.

Akifungua Kongamano la Sera na Mitaala ya Elimu kuhusu  uhuishaji wa Sera na Mitaala ya Elimu leo Mei 12,2023 jijini Dodoma,Waziri wa Elimu,Sayansi na Tekonolojia Profesa Adolf Mkenda amesema,mapendekezo ya kufufua shule za sekondari za ufundi ni kutokana na vijana wengi kuona kama kusoma ufundi bila kuwa na elimu ya sekondari wananyanyapaliwa .

“Tumetenga bajeti ya kurudisha shule zetu za sekondari ambazo pia zinafundisha masomo ya ufundi ,hii ni kwa sababu tumeona vijana wengi wakienda kusoma katika vyuo vya ufundi,wanarudi tena kufanya mtihadi wa kidato cha sita ili waende vyuo vikuu,wakidhani kusoma ufundi ni kama kujidhalilisha.”amesema Prof.Mkenda

Aidha amesema,katika mapendekezo ya sera mpya ya Elimu na Mitaala serikali imependekeza elimu ya msingi iwe kwa kipindi cha miaka 6 badala ya saba ya sasa , lakini pia mwanafunzi lazima asome shule ya msingi na sekondari (O-Level) huku akisema  ,mapendekezo kuhusu utekelezaji wa Sera hiyo mpya utawekwa katika kalenda kwa ajili ya kuanza kutumika kwa majaribio  Januari mwakani.

“Elimu ya sekondari itakuwa na mikondo miwili ambayo ni  Elimu ya Jumla na Elimu ya Amali yaani ufundi na ufundi stadi  ambapo katika elimu ya Amali wanafunzi watafundishwa  ufundi kwa vitendo ambapo kila mkondo utakuwa na michepuo.”amesema Prof.Mkenda

Akizungumza kuhusu namna ya kupata walimu aliwatoa wasiwasi walimu waliopo kazini huku akisema utaratibu huo hautawahusu na badala yake Serikali itatoa fursa kwa waliopo sasa katika ajira kujiendeleza na kwamba watafanya kazi mpaka watakapostaafu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Profesa Caroline Nombo alisema,Katika utekelezaji wa rasimu hiyo kulikuwa na kmati mbili ambazo zimefanya kazi ya kukusanya maoni ambapo zaidi ya wadau 200,000 walifikiwa na kupata fursa ya kutoa maoni yao kuhusu maboresho ya sera na  mitaala ya elimu hapa nchini .

“Sera hiyo na Mitaa haijaangalia tu wakati uliopita ili imechambua hali halisi iliyopo kwa sasa katika elimu yetu kuanzia elimu ya awali,msingi,sekonda mpaka elimu ya ualimu.”amesema Profesa Nombo

Awali Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu,Utamaduni na Michezo Profesa Kitila Mkumbo  amesema,kongamano hilo ni fursa kwa wabunge kuchukua maoni na kuyafanyia kazi ili kuhakikisha serikali inayachukua lakini pia kwa yale ya kisheria,Kamati hiyo itahakikisha Sheria inatungwa .

“Kumekuwa na changamoto katika mfumo wetu wa Elimu,ndiyo maana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameelekeza ufanyiwe kazi kwa ajili ya kupata sera na mitaala bora itakayowezesha wahitimu kujiari na kuisaidia jamii na Taifa kwa ujumla.”amesisitiza Prof.Mkumbo

Serikali imekuwanisha wadau wa Elimu ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kupitia na kutoa maoni ya mwisho katika Rasimu ya Sera ya Elimu na Mafunzo  ya 2014,toleo la 2023 ili kupata sera ya Elimu na Mafunzo inayotarajiwa kuanza kutumika mwakani.