May 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kampuni zatakiwa kufanya kazi kwa weledi, uaminifu

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji NIRC, Raymond Mndolwa, ametoa wito kwa kampuni zilizoshinda zabuni za kufanya upembuzi yakinifu katika mabonde 22 ya kimkakati nchini kufanya kazi kwa weledi na uaminifu.

Mdolwa amesisitiza kuwa zoezi hilo linapaswa kuwashirikisha wadau wote katika maeneo husika, ikiwa ni pamoja na wenyeviti wa vijiji, viongozi wa skimu na wakulima wa maeneo hayo.

Akizungumza jijini Dodoma na wakurugenzi wa makampuni zaidi ya sita, Mdolwa amewataka wahandisi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji waliopo maeneo yanayotekelezwa zoezi hilo kufanya kazi kwa pamoja na makampuni hayo ili kuhakikisha zoezi hilo linafikia malengo yaliyokusudiwa.

Wakurugenzi wa makampuni hayo nao wameahidi kutekeleza zoezi hilo kwa weledi na ufanisi.

Miongoni mwa maeneo yanayohusika na zoezi hilo ni pamoja na Bonde la Ziwa Victoria, Ruvuma Songwe na Kilombero.

Mdolwa amesema lengo la kukutana na wakurugenzi wa kampuni hizo ni kujenga uelewa wa pamoja kurahisisha utendaji na kupata matokeo chanya.

“Ni matumaini ya wadau wote kwamba zoezi hilo litakamilika kwa ufanisi na kusaidia katika kuboresha kilimo na umwagiliaji nchini.”