April 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Yanga yaendelea kugawa dozi, yaichapa Geita Gold kwao, kituo kinachofuata KMC

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

TIMU ya Yanga Sc imeendeleza wimbi la ushindi katika Ligi kuu Tanzania bara baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1- 0 dhidi ya Geita Gold ndani ya dimba la CCM kirumba mwanza.

Bao la mapema kutoka kwa Kinara wa mabao Fiston Mayele ambaye amefikisha bao lake 10 katika ligi alitumia vizuri makosa ya walinzi wa Geita Gold liliwapa uongozi wananchi katika dakika 45 za kipindi cha kwanza.

Kipindi cha Pili Geita Gold walirejea kwa kasi kutafuta bao la kusawazisha na kutengeneza nafasi kadhaa lakini kukosekana kwa umakini kwa washambuliaji wao na uimara wa safu ya ulinzi ya Yanga uliwanyima nafasi ya kupata bao la kusawazisha ili kupata angalau alama moja katika Uwanja wao wa nyumbani.

Benchi la ufundi la Yanga lilifanya mabadiliko kadhaa kuimarisha eneo la kiungo, Denis Nkane na Paul Godfrey walitolewa na nafasi zao kuchukuliwa na Zawadi Mauya na Dikson Ambundo, na baadae mshambuliaji Fiston Mayele alipata majeraha na nafasi yake kuchukuliwa na Heritie Makambo .

Baada ya ushindi huo Yanga sasa imefikisha alama 45 baada ya kushuka dimbani mara 17 wakifuatiwa na wapinzani Simba wenye alama 34 kwenye mechi 16 leo watashuka dimbani dhidi ya Dodoma Jiji katika dimba la
Benjamini Mkapa Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kukamilika kwa mchezo kocha wa Yanga Sc Nesredin Nabi amesema kuwa mpango wa timu ulikuwa ni kupata mabao mengi zaidi na kutengeneza mazingira mazuri ya kuondoka na alama 3.

” Hatukuwa na lengo la kuzia lakini bao la mapema liliwapa nguvu wapinzani wetu na kutaka kusawazisha , nashukuru wachezaji wangu wamefata maelekezo sasa nguvu kubwa tunazielekeza katika mechi zinazofuata” alisema kocha Nabi

Kwa upande wake kocha wa Geita Gold Fred Felix Minziro aliwapongeza wachezaji wake kwa kuonesha kiwango bora mbele ya vinara wa ligi huku akikiri ukosefu wa umakini kwa wachezaji wake uliwanyima fursa ya walau kupata alama 1.