April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Spika amwaga milioni 78/- kwa
wanawake wajasiriamali Mbeya

Na Esther Macha, TimesMajira,Online Mbeya

SPIKA wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini, Dkt.Tulia Ackson, kupitia Taasisi yake ya Tulia Trust ametoa mItaji ya biashara kwa wajasirimali wanawake 601 wa Mkoa Mbeya yenye thamani ya sh. milioni 78.1.

Dkt. Tulia ametoa mitaji hiyo leo katika hafla iliyofanyika jijini Mbeya, ambapo walengwa ni wanawake wajasariamali ambao wanafanya biashara zao sokoni .

Aidha, Dkt. Tulia amesema wale waliowezeshwa mwaka jana wamefanya utafiti na asilimia 75 kati yao wanaondelea vizuri na ni asilimia 25 ya waliopewa mitaji ambao hawakufanya vizuri .

“Tunaamini kuwa akina mama 601 ambao tutawezesha leo mtatufanya tuongoze juhudi zaidi kwa sababu mwaka jana tuliwezesha akina mama 309 sawa na asilimia 75 tu, wameweza kuendelea, lakini hiyo si asilimia ndogo kwa sasabu lengo letu ni kuona wanawake wanatoka hatua moja kwenda nyingine, tunatamani kuona asimilimia 100 mnafanya vizuri zaidi na nyinyi wa mwaka huu tumeongeza idadi akina mama 500 wanatoka Mbeya ,akina mama wengine 100 wanatoka wilaya zingine ambazo ni Kyela ,Mbarali ,Chunya , Rungwe na Mbeya Vijijini,” amesema Dkt, Tulia.

Akifafanua zaidi Dkt. Tulia amesema akina mama 601 waliopewa mitaji hiyo wasimwangushe, wafanye bidii kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassan ambaye anatamani wanawake wote wawe wa mfano kwenye jamii .

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mbeya, Afrey Nsomba amesema chama kinamwamini na kwamba amefanya kazi nyingi bila kuchagua itikadi za vyama .

Hata hivyo, amesema Dkt.Tulia ni mfano wa kuigwa kwani hata kabla hajawa mbunge wala spika alifanya kazi nyingi za kujitoa na kulibadilisha Jiji la Mbeya, hivyo watahakikisha wanamsaidia.

Amesema kuwa mitaji hiyo sio mikopo bali ametoa bure ambapo kwa Mwakani watawafuatilia ili kuona mienendo ya biashara zao na watakaofanya vizuri wataongezewa.

“Kila mmoja anapata sh. 100,000 na ili waongeze mitaji yao na sh. milioni 1 ni kwa ajili ya mashine ambayo ni kwa ajili ya wanawake ambao wanajishughulisha na ukamuaji wa mafuta ya alizeti,”amesema.

Mkuu wa Wilaya Mbeya, Dkt. Rashid Chua amesema mbunge huyo ni nuru kwa wananchi wa Mkoa wa Mbeya hivyo wamuombee ili aweze kuwatumikia na kuwawezesha kiuchumi.

“Mkoa wa Mbeya kuwa na Spika ni Bahati kutoka kwa Mwenyezi Mungu na sisi kama viongozi wa Serikali tutakuwa naye bega kwa bega kuhakikisha Mkoa unapiga hatua za maendeleo,”amesema.

Naibu Meya wa Jiji la Mbeya, Agnes Mangasira amesema kitendo alichofanya Spika kwa wanawake wajasirimali ni kikubwa hivyo ni vyema wanawake waliopewa mitaji hiyo wakafanye vizuri katika biashara zao na wasimwangushe Mbunge wao.

“Ndugu zangu wanawake hii dhahabu tuliyopewa tuitunze na kuiombea ili iweze kufanya vizuri zaidi ni nuru kwetu wana Mbeya kwani hata Jiji letu la Mbeya limebadilika,”amesema Naibu Meya.