May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

WRRB yatoa mafunzo ya utekelezaji wa mfumo wa stakabadhi za ghala

Na Penina Malundo

BODI ya usimamizi wa stakabadhi za ghala (WRRB) yatoa mafunzo ya utekelezaji wa mfumo wa stakabadhi za ghala yenye lengo la kuwajenga uwezo Watendaji wa Kampuni za waendesha ghala, Wasimamizi wa Ghala, Meneja Dhamana pamoja na washiriki binafsi.

Akizungumza leo Mkuu wa wilaya ya Ubungo, Hashim Komba katika ukumbi wa Kilimanjaro uliopo katika Uwanja wa Maonesho ya Sabasaba,alisema mafunzo hayo yanakwenda kuongeza heshima kwa watendaji wa ghala na kupelekea utoaji wa huduma bora kwa Wadau wote.

Amesema bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala inatakiwa kuongeza matumizi ya TEHAMA katika utendaji ili kuendana na mabadiliko ya dunia.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Stakabadhi za Ghala Asangye Bangu amesema kuwa lengo kubwa la mafunzo hayo ni kuongeza tija katika ufanyaji kazi na matarajio ya mafunzo hayo ni kuhakikisha kazi zinafanywa kwa usahihi kwa kuzingatia sheria .

Bangu ameongeza kuwa Bodi ya Udhibiti na Usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala imejipanga kuona ambavyo watendaji hao watatekeleza shughuli zao za kiserikali kwani wamejitaidi kuingiza bidhaa mbalimbali kadiri sheria ilivyo waruhusu kufanya hivyo.