May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

MWAUWASA yaiomba TANESCO kuwa na line mahususi kwa ajili ya mitambo ya maji

Judith Ferdinand, Timesmajira Online, Mwanza

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) Neli Msuya,ameiomba TANESCO kuwa na line mahususi (dedicated line) kwa ajili ya mitambo mipya eneo la chanzo kipya cha maji Butimba na vituo vya kusukuma maji (booster stations).

Kaimu Mkurugenzi huyo ambaye kwa
nyakati tofauti amefanya ziara yakutana na wadau muhimu wa sekta ya maji jijini Mwanza ikiwemo TANESCO ili kujadili namna ya kuboresha hali ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Jiji hilo.

Awali alikutana na Meneja wa TANESCO Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Godlove Mathayo na kujadili hatua mbalimbali za ushirikiano ili kuhakikisha huduma ya maji jijini Mwanza inaimarika na katika majadiliano hayo alitumia fursa hiyo kuiombea TANESCO kuwa na line mahususi kwa ajili ya mitambo ya uzalishaji maji.

Msuya amesema kuwa kwa kiwango kikubwa shughuli za uzalishaji maji zinategemea nishati ya umeme kutoka Tanesco,hivyo ni muhimu kuimarisha ushirikiano ili kupunguza changamoto ya upatikanaji maji katika jiji la Mwanza.

“Sisi kama watoa huduma kwa jamii, ni vyema tushirikiane,naamini tukiboresha upatikanaji wa umeme hata upatikanaji wa huduma ya maji utaimarika kwa kuwa mitambo yetu ya uzalishaji inaendeshwa kwa nishati ya umeme,”amesema Neli.

Aidha kwa nyakati tofauti Kaimu Mkurugenzi huyo wa MWAUWASA amekutana na Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria, Renatus Shinhu na kuiomba bodi hiyo kufanya utafiti wa maji chini ya ardhi maeneo ya pembezoni na yenye changamoto ya maji ikiwa ni suluhisho la muda wakati miradi mikubwa ikijengwa.

Wadau hao wa MWAUWASA kwa nyakati tofauti wamemuahidi Mkurugenzi Neli ushirikiano wa kutosha katika kuwaimarishia huduma ya maji wananchi wa Mwanza.