April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu

Waziri Ummy: Ugonjwa wa Corona unaelekea kuisha nchini

Na Penina Malundo, TimesMajira Online

WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,Ummy Mwalimu amesema ugonjwa wa Corona unaelekea kuisha nchini ambapo hadi sasa mikoa zaidi ya 15 haijaripoti mgonjwa yeyote kwa zaidi ya wiki.

Waziri Ummy amesema hayo wakati alipotembelea kituo cha afya cha Mkonze kilichotengwa kwa ajili ya kuwahudumia watu waliopata maambukizi ya ugonjwa wa Corona jijini Dodoma na kukuta vitanda vikiwa tupu bila kuwa na mgonjwa yeyote kwa zaidi ya wiki.

Kupitia Waganga wakuu wa Mikoa 15 nchini, wamethibitisha kutokua na mgonjwa wa Corona huku Mikoa mingine yenye wagonjwa ikiripoti wagonjwa hao kuendelea vizuri.

“Nawashukuru watoa huduma za afya wa kituo cha Mkonze kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kuwahudumia wagonjwa na kuchukua tahadhari zilizosaidia wahudumu hao kutopata maambukizi ya Corona,” amesema Waziri Ummy.

Licha ya ugonjwa wa Corona kuelekea kumalizika nchini, amewataka wananchi kutobweteka na kuendelea kuchukua tahadhari kwa kuzingatia maelekezo yanayotolewa na wataalam wa afya ikiwemo kunawa mikono mara kwa mara kwa sabuni na maji tiririka pamoja na kuvaa barakoa za vitambaa wanapokua kwenye mikusanyiko.