April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Asia Mkene Afisa Ustawi wa Jamii Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mwananyamala akitoa huduma kwa mwananchi aliyefika kwenye hospitali hiyo katika maonesho ya maadhimisho ya wiki ya magonjwa yasiyoambukiza kwenye viwanja vya mnazi mmoja yaliyofanyika jijini Dar es Salaam,kulia ni Koplo Salome Izina

Wazazi watakiwa kuimarisha ulinzi kwa watoto

Na. Mwandishi Wetu,TimesMajira,Online

MUUGUZI  Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mwananyamala,Musa  Maroko amewataka wazazi nchini kuwa walinzi wa watoto ili kukabiliana na ukatili wa kijinsia kwenye jamii.

Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam wakati wa maonesho ya wiki ya magonjwa yasiyoambukiza yaliyomalizika mwishoni mwa wiki  hii viwanja vya mnazi mmoja.

Maroko amesema kuwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia  pamoja na ukatili kwa watoto bado vinaongezeka miongoni mwa jamii kila siku.

“Kutokana na hali hiyo hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mwananyamala imeanzisha huduma jumuishi  kwa ajili ya kuwasaidia wahanga hususani wakazi wa Kinondoni, Ubungo na Dar es Salaam kwa ujumla”amesema

Amesema  lengo la kuanzisha huduma hiyo ni kuwasaida wananchi ambao hawawezi kwenda polisi hivyo kituo hicho kinawasaidia kupata huduma nne kwa pamoja ikiwemo ya kisheria,kitabibu,kipolisi na ustawi.

“Mtu anapopata tatizo la kingono anapaswa kutopoteza ushahidi ili kuweza kuwa rahiai  kushughulikia tatizo hilo,kwahiyo akifika ataonwa na ushahidi utawekwa kwa kufuata taratibu zote za kisheria na kuhifadhiwa kwa usalama,”amesema

Naye Koplo Salome Izina kutoka kituo hicho amesema huduma hiyo imekuwa na mafanikio kwenye kanda yao kwani inampunguzia gharama mwananchi na kuweza kupata vielelezo vilivyo sahihi kutoka maabara kwenye hospitali hiyo.

 Koplo Izina  amewataka wazazi kutochelewa kutoa taarifa mara baada ya kujua tatizo limetokea  ili kupata ushahidi mzito wa kuweza kumuunganisha na mtuhumiwa.

Wakati huohuo Afisa Ustawi wa Jamii wa hospitali ya rufaa ya Mkoa ya Mwananyamala ,Asia Mkene amesema bado wanawake wengi wananyamaza wanapofanyiwa ukatili wa kijinsia na sababu kubwa ni kutokuwa na elimu ya kutosha na hivyo ushindwa kuripoti. Amesema  kituoni hapo asilimia 87 za kesi wanazopokea ni za watoto ikifuatia wanawake huku  kesi za kinababa zikiwa na asilimia ndogo