May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watuhumiwa wa mauaji wifi na mwenzake kizimbani

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online,Mwanza

Mkazi wa Dar es salaam, Elizabeth Josephat Ndakidemi (35) na Faida Daud Masaba (24), Mkazi wa Igoma wilayani Nyamagana Mkoa wa Mwanza wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Wilaya ya Ilemela mkoani hapa na kusomewa shtaka la mauaji.

Washtakiwa hao wamesomewa shtaka hilo katika kesi ya Jinai namba 40349/2023 ambapo wote kwa pamoja wanadaiwa kushirikiana kumuua, Flora Philimon Bibwa kinyume na Kifungu namba 196 na 197 ya Sheria ya Kanuni ya Adhabu sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2022.

Akisoma mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilemela, Fortunatus Kubaja, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Monica Mweli amesema washtakiwa walitenda kosa hilo Novemba 13,2023, eneo la Nyamh’ongolo wilayani Ilemela mkoani Mwanza.

Baada ya kusomewa shtaka hilo, washitakiwa hawakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka kisheria ya kusikiliza kesi hiyo na shauri hilo limeahirishwa hadi Januari 4, mwaka 2024.