May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watiwa mbaroni kwa tuhuma za mauaji

Na Daud Magesa, Timesmajira online, Mwanza

JESHI la Polisi Mkoa wa Mwanza linawashikilia watu watatu wakiwemo wanawake wawili wa familia moja kwa tuhuma ya mauaji ya mkazi mmoja wa Nyakabungo jijini hapa,Peter Dominic almaarufu Mang’ela.

Akizungumza na waandishi wa habari,Mei 26,mwaka huu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza,Wilbroad Mutafunga ,amesema wanawashikilia watu hao kwa tuhuma za kuhusika na tukio la mauaji ya Dominic maarufu Mang’ela, lilitokea Mei 25, mwaka huu, majira ya saa 3:30 usiku huko maeneo ya Nyakabungo wilayani Nyamagana,jijini Mwanza.

Mutafungwa amesema marehemu alikwenda nyumbani kwa Julius Gain ambaye ni jirani yake, kudai deni la fedha zake kiasi cha shilingi6,500 baada ya kumuuzia pombe ya kienyeji ndipo ukatokea ugomvi.

Ameeleza katika ugomvi huo marehemu Dominic alishabuliwa kwa kupigwa na kitu chenye ncha kali na kusababisha kuvuja damu nyingi hatimaye kupoteza maisha ambapo polisi walifika na kuwatia mbaroni watuhumiwa.

Kamanda huyo wa polisi amewataja wanaoshikiliwa kwa mauaji hayo kuwa ni Julius Gain (59),Judith John (48) na Roda Julius (49), wote wa familia moja na wakazi wa Nyakabugo na baada ya upelelezi kukamilika watafikishwa mahakamani.