May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wateja TPB kunufaika na bima ya maisha, kuzoa mamilioni na wategemezi wao

Na Prona Mumwi, TimesMajira,Online Dar

BENKI ya TPB imeingia makubaliano na Kampuni ya Bima ya Alliance life Assurance kwa ajili ya kutoa bima ya maisha kwa wateja wenye akaunti binafsi katika benki hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mkoani Dar es Salaam katika hafla hiyo, Mkurungezi wa TPB, Sabasaba Moshingi amesema bima hiyo itatolewa kwa wateja wenye akaunti binafsi kwenye benki hiyo dhidi ya tukio la kifo cha mteja, mwenza na ulemavu wa kudumu wa mteja unaotokana na ajali.

Amesema kifi mteja atapata sh. milioni 2 na mwenza wa mteja kiasi hicho hicho. Kwa upande wa watoto wa mteja, wasiozidi wanne kila mmoja sh. milioni 1.

Kwa upande wa fao la ulemavu wa kudumu, Moshingi alisema linatolewa kwa mwenye akaunti ambapo atapata sh. milioni 2.

Amesema benki hiyo imekuwa ikitambua umuhimu wa bima katika maisha ya binadamu, hivyo imeona ni vema kuungana na Kampuni ya Alliance life Insurance kuwawezesha wananchi kupata huduma hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Posta TPB Saba saba Moshingi (kulia) akibadilishana hati ya makubaliano na Mkurungezi kutoka Kampuni ya Alliance life Assurance, Byford Mutimusakwa,(kushoto) baada ya kuzindua Bima ya Maisha kwa wateja wa benki hio. Hafla hiyo imefanyika jijini Dar es Salaam jana. Picha na Prona Mumwi

“Benki ya TPB imekuwa ikitambua umuhimu wa bima katika maisha ya binadamu na kwa sasa nchi yetu imekuwa ikikabiliwa na ufinyu wa watu katika kujiandikisha katika bima mbalimbali,”amesema

Moshingi amesema huduma hizo hazitakuwa na gharama ya juu kwa mteja, huku akisisitiza kuwa mafao hayo ni kwa ajili wamiliki na mmiliki wa akaunti tu na mteja ni lazima awe na akaunti ya akiba na iwe hai.

Awali Mkuu wa kitengo cha Bima TPB, Francis Kaaya amesema katika bima hiyo kutakuwa kukitolewa mafao mawili ambayo ni pamoja na fao la kifo na fao la ulemavu wa kudumu.

” Fao la kifo ni fao kwa wateja wenye akaunti za akiba dhidi ya tukio la kifo cha mmiliki wa akaunti, mwenza na watoto wasiozidi wa nne,”amesema Kaaya

Na kuongeza kuwa TPB itatoa kifuta machozi kwa mteja au familia Kama rambirambi ili kutatua baadhi ya gharama zinazohusu mazishi.

Katika fao la ulemavu wa kudumu, Kaaya amesema hili fao ambalo litapatikana kwa mteja au wateja ambaye ni mmiliki wa akaunti anayekabiliwa na ulemavu wa kudumu uliotokana na ajali.

Kwa upande wake Mkurungezi kutoka Kampuni ya Alliance life Assurance, Byford Mutimusakwa amesema bima ni muhimu katika maisha kila mtu hivyo ameipogeza benki ya TPB kwa kuhakikisha wateja wake wanapata huduma hiyo.

“Kwa sasa wateja wa benki ya TPB wataweza kupata bima hii ya nishike mkono pasipo na usumbufu wote,”amesema

Aidha amewataka wananchi kuwa na tabia ya kutumia bima ili kuepuka majanga mbalimbali katika maeneo wanayoishi na wanayofanya kazi.