May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu

Watanzania watakiwa kujilinda kikamilifu

Na Penina Malundo

WAGONJWA wengine wapya 14 wamethibitika kuwa na maambukizi ya Corona Tanzania Bara na kufanya idadi ya wagonjwa hao kufikia 46 kutoka 32 waliotolewa taarifa Aprili 10, mwaka huu.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa Dar es Salaam jana na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, imeeleza kuwa kati ya wagonjwa hao hao wapya, 13 wapo Dar es Salaam na mmoja Arusha.

“Wagonjwa wote wanaendelea na matibabu chini ya uangalizi wa wataalam wa afya. Ufuatiliaji wa watu waliokuwa karibu na wagonjwa unaendelea,” alisema Waziri Ummy.

Kupitia taarifa hiyo Serikali imerudia kuwasisitiza wananchi kuchukua tahadhari ya kujikinga na ugonjwa huu kama wanavyopata taarifa na elimu mara kwa mara kupitia njia mbali mbali na hasa kuepuka misongamano na mikusanyiko isiyokuwa ya lazima.

***Hali ya Zanzibar

Kwa upande wa Zanzibar idadi ya wagonjwa wa ugonjwa huo imezidi kuongezeka nako baada ya kuthibitika kupatikana wagonjwa wapya watatu.

Taarifa iliyotolewa jana na Waziri wa Afya – Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed, ilieleza kwamba jana walipokea majibu ya sampuli walizopeleka juzi kwa ajili ya uchunguzi.

Alisema sampuli hizo tatu zimeonekana kuwa na maabukizi ya ugonjwa wa Corona. “Hii inafanya idadi ya wagonjwa wetu hadi sasa kuwa 12 baada ya ongezeko la wagonjwa watatu wapya.

“Hadi kufikia leo (jana) tuna jumla ya wagonjwa 12 waliolazwa katika kituo maalumu cha matibabu cha Kidimni na kile cha Skuli ya JKU Mtoni kilichofunguliwa hivi karibuni kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa wa Corona,”alisema Mohamed.

Alisema wagonjwa wanaendelea vizuri na afya zao zinaendelea kuimarika siku hadi siku.

Aliongeza kuwa wagonjwa wawili waliokuwa wakipatiwa matibabu katika kituo cha Kidimi wamepona na kuruhusiwa kurudi nyumbani, huku wakitakiwa kuendelea kubaki ndani bila ya kuchanganyika na watu wengine kwa siku 14.

Akifafanua zaidi kuhusu wagonjwa walioongezeka, Waziri Mohamed alisema wote ni Watanzania, wa kwanza akiwa ni mwanamme wa miaka 30, mkazi we Mwanakwerekwe aliyeripotiwa Aprili 10, mwaka huu.

Alisema mgonjwa huyu alikuwa karibu sana na mmoja kati ya wagonjwa wa awali waliolazwa Kidimni.

Mgonjwa wa pill  alisema ni mwanamme mwenye umri wa miaka 22, mkazi wa Jang’ombe mjini Zanzibar. Alisema aliripoti hospitali Aprili 8, mwaka huu akiwa na homa kali na kikohozi na alipochukuliwa kipimo aligundulika kuwa na maambukizi ya virusi vya Corona.

“Mgonjwa wa tatu naye ni mwanamme miaka 19, mkazi wa Bumbwisudi aliyeripotiwa Aprili 10, mwaka huu akiwa na homa kali na kikohozi na baada ye kuchukuliwa kipimo naye alionekana kuwa na maambukizo,” alisema Waziri huyo.

Alisema wagonjwa wote hao hawana historia ya kusafiri nje ye nchi katika siku ze hivi karibuni. “Hii inathibitisha kwamba maradhi haya sasa tayari yamo kwenye jamii yetu na hivyo kuongeza hatari ya kuambukizana wenyewe kwa wenyewe endapo tahadhari ze ziada hazikuchukuliwa,” alisema Waziri Mohamed.

Alisema Wizara ya Afya inaendelea kufuatilia watu wa karibu waliowahi kukutana na wagonjwa hawa ili kudhibiti kuenea kwa maambukizi mapya na hadi kufikia jana Aprili 12, 2020, jumla ya  watu 164 waliokutana na wagonjwa wa maradhi hayo na wanaendelea kufuatiliwa.

Aidha, alisema jumla watu 232 waliotoka safari za nje ye nchi wamewekwa Karantini Unguja ne Pemba ne wengine 264 wameruhusiwa kutoka Karantini hizo baada ya kumaliza siku 14 bila ya kuonesha dalili za maradhi haya.

“Wito wangu kwa wananchi ni kwamba, hali ya maambukizo ya maradhi haya hapa nchini bado ni tete kwani, hatujui wangapi kati yetu wameambukizwa,” alisema na kuongeza;

“Hatuna budi kila mmoja wetu achukue tahadhari za ziada kuhakikisha tunakatisha mnyororo huu wa maambukizo. Tuzingatie maelekezo yanayotolewa na Serikali na wataalam.”

Alitaja mambo ambayo yanatakiwa kuzingatiwa kuchukua tahadhari kuwa ni pamoja na kuongeza bidii katika kunawa mikono mara kwa mara na kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima, kuepuka misongamano katika vyombo vya usafiri kwa kupunguza idadi ya abiria kadri inavyo wezekana.

“Tuchukue tahadhari za ziada mara zote tunapoenda katika masoko au vituo vya daladala. Inashauriwa sana kuvaa maski kila tunapoenda katika maeneo haya na kila inapobidi kukaa basi tuweke masafa ya angalau mita moja na nusu  hadi mbili baina ya mtu na mtu,”alisema.

Alitaka wananchi wazidi kuchukua tahadhari katika maeneo ya ibada pamoja na kufuata maelekezo yote yanayotolewa na viongozi wetu wa dini kupitia Baraza la Maulamaa na Baraza la Maaskofu Nchini.

Hatua zingine za kufuata ni taasisi zote za Serikali na zisizo za Serikali zisimamie vyema maagizo ya Serikali juu ya kinga ya maradhi haya ikiwemo kuweka miundombinu sahihi ya kinga katika maeneo yao.

“Ni vyema tukachukuwa tahadhari za kutosha sasa kuliko kusubiri athari kubwa za janga hill kama inavyoonekana katika nchi za wenzetu, zikiwemo zile zenye nguvu na uwezo mkubwa duniani,” alisema.