April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watakiwa kutenga siku ya maombi

Na Esther Macha,Timesmajira,Online,Mbeya

WACHUNGAJI na waimbaji wa nyimbo za injili Jijini Mbeya wameshauriwa kutenga siku maalum kwa ajili ya maombi kwa Taifa.

Wito huo umetolewa na na Mkurugenzi wa Shule za Paradise Mission&Primary iliyopo Mji Mdogo wa Mbalizi katika Kata ya Nsalala,Ndele Mwaselela, alipokuwa akizungumza wakati chakula cha jioni alichoandaa kwa ajili ya waimbaji wa nyimbo za injili wa Mkoa wa Mbeya.

“Niwaombeni na nyie wachungaji kupitia waimbaji wenu mtenge siku maalum za maombi kwa Mkoa wa Mbeya, kwa sababu Taifa hili linahitaji maombi, tusijifanye tumemaliza kila kitu.

Rais Samia Suluhu Hassan kule juu anasema tuombe, wakuu wa mikoa wanasema tuombe, wakuu wa wilaya pamoja na wakurugenzi ni nyie ndio mumeshika mpini, mimi siwezi kusema tuombe sina kola ndugu zangu zaidi  mimi nitawaambia pelekeni watoto shule nilichosema muungane sasa kwenye ratiba zenu mtenge siku maalum za maombi mkoa wa mbeya,”amesema.

Amesema wakifanya hayo Mungu atawapenda na duniani mtapendwa kwa sababu hakuna mtu asiyependa maombi na mtu akipatwa na shida tu lazima akimbilie maombi.

Mkurugenzi paradise Mission, Ndele Mwaselela akizungumza na waimbaji wa nyimbo za injili jijini hapa.

Akifafanua zaidi amesema kuwa hakuna mtu ambaye amewahi kudharau maombi hata siku moja kuanzia mlevi hadi mtu wa barabarani, hivyo maombi  yana nguvu na hakuna mjanja hata siku moja.

“Nilikuwa namwambia mchungaji hapa kuwa wakiwa mazabauni wakibahatika kutembelewa na watu mitaani huwa wanatoa sadaka nzito nzito wakijua wanatubu kweli,”amesema.

Aidha  Mwaselela amesema umoja huo usife tena kwani huo ni umoja wa waimbaji wa nyimbo za Injili  ambao utaweza kuwatambulisha katika maeneo mbalimbali.

Baadhi ya waimbaji wa nyimbo za injili wakimsikiliza mkurugenzi huyo.

“Umoja huu utakuwa na ndoto kubwa na uwe na nguvu na mfano kwa waimbaji wa  nyimbo za injili wengine wa mikoa mingine,kwenye umoja huu lazima tubuni kitu kinaitwa tamasha la dini la waimbaji wa nyimbo za injili asitokee mtu anataka kuandaa peke yake.

Tunataka kuutangaza mkoa wetu vizuri kwa nyimbo zenye kuleta ujumbe wa kisiasa,”amesema.

Akizungumzia kuhusu siri za umoja huo Mkurugenzi wa Paradise Missioni amewataka  waimbaji kutunza siri za masuala ya msingi ya maadili ya umoja, asitokee mtu hata mmoja akatoa siri za umoja.

“Nataka kuanzia mwezi huu umoja wa waimbaji mkoa wa Mbeya ufanye kazi ya kutengeneza umoja wenye nguvu kwa mara kwanza hivyo mimi nitajitolea ukumbi na chakula.

Tutawaita watu mbali mbali ambao ni viongozi wakubwa wa mkoa na kutambulisha umoja wetu na tuone wametuacha wapi,”amesema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa umoja wa waimbaji Mkoa wa Mbeya , Tumaini Mbembela amemshukuru mkurugenzi huyo kwa kuwakusanya pamoja waimbaji wa injili wote wa mkoa wa Mbeya na kuwaweka pamoja ili waweze kufanya vitu vya msingi katika kuimarisha umoja wao.

Kwa upande wake Charles Mwakipesile ambaye ni mlezi wa waimbaji wa nyimbo za injili Mkoa wa Mbeya amesema wapo watu wengi wenye fedha, lakini hawajaweza kudhubuti kuwaweka pamoja.

Mkurugenzi wa shule za paradise Mission na Patrick zilizopo Jijini Dar es Salaam katika kufanikisha adhima yake ya kuyaunganisha pamoja makundi mbali mbali Jijini Mbeya tayari ameahidi kununua Coaster kwa ajili ya waandishi wa habari.