April 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wasimamizi wa uchaguzi watakiwa kutozima simu zao

Na Tiganya Vincent, Tabora

WASIMAMIZI wa Uchaguzi wa Mikoa na Wasimamizi wa Uchaguzi Mkuu ngazi ya Wilaya na Majimbo wameagizwa kuhakikisha simu zao zinakuwa wazi katika kipindi chote hadi uchaguzi utakapomalizi na matokeo kutangazwa rasmi na Tume ya Uchaguzi.

Hayo yamesemwa na mjini Tabora na Afisa kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC) Edward Makono wakati wa Mafunzo kwa wasimamizi hao wa uchaguzi 110 toka mikoa na Kigoma na Tabora.

Amesema lengo la kuwataka simu zao kuwa wazi ni kuhakikisha kuwa wanakuwa tayari kila wakati kupata maelekezo yanayohusu masuala ya uchaguzi na upokeaji wa vifaa vya uchaguzi pindi vitakapoanza kugawanya katika maeneo mbalimbali katika maeneo wanayosimamia.

“Mkiwa wasimamizi wa uchaguzi wanatakiwa kuwa tayari wakati wote hata ikibidi kupunguza baadhi ya shughuli binafsi ambazo zinaweza kuathiri uchaguzi…mnapolala …lala ukiwa tayari na wala usizime simu yako wakati wote” amesisitiza.

Amesema kitendo cha kuzima simu kinaweza kusababisha msambazaji wa vifaa vya uchaguzi kuchelewa kufika katika vituo vinavyofuata na hivyo kuchelewesha zoezi la uchaguzi.

Makono amesema msimamizi yoyote ambaye atasababisha vifaa vichelewe kupokelewa kwa simu ya simu yake kutopatikana atachukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria za Uumishi wa umma na zile za Tume ya Uchaguzi (NEC).