April 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wasichana wa kazi za ndani walalamikia ukosefu wa mikataba

Na Rose Itono,timesmajira,Online

BAADHI ya wasichana wa kazi za ndani wamesema kukosekana kwa mikataba ya ajira za kazi zao kunachangia baadhi yao kutoa rushwa ya ngono kwa waajiri wao wa kiume ili kulinda kazi zao.

Wakizungumza kwenye semina ya kuwajengea uwezo wasichana wanaifanya kazi za ndani iliyoandaliwa na Taasisi ya Sauti ya Jamii Kipunguni kupitia ufadhili wa Dar es Salaam jana walisema kukosekana kwa mikataba ya kazi na elimu ya kujitambua kunachangia kujiingiza kwenye vitendo hivyo

Latifa Mussa mkazi wa Chanika mmoja wa wasichana aliyeshiriki semina hiyo amesema vitisho wanavyopewa baadhi ya wasichana na mabosi zao wa kiume vinasababisha wengine kutoa rushwa ya ngono

” Wakati mwingine tumekuwa tukijaribu kukataa kushiriki mapenzi na mabosi zetu wa kiume lakini wamekuwa wakitupa vitisho na kulazimika kushiriki nao bila Kupenda, “amesema Mussa

Amesema elimu ya kujitambua inahitajika kwa wasichana wa kazi ili kuwawezesha kuwa na maamuzi sahihi ya maisha yao

Mariam Mussa msichana mwingine ameongeza kuwa mbali na vitendo hivyo kufanywa na mabosi zao wa kiume pia mabosi zao wakike wanachangia kwa kiasi kikubwa kutokana na kutokuwa karibu na wasichana wao wa kazi

” Ukijaribu kutaka kumueleza bosi wako wa kike kuhusu muenendo mbaya anaotaka kuufanya bosi wa kiume kesi yote inahamia kwako, ukiangalia una shida na kazi na hivyo kujikuta ukilazimika kutoa rushwa ya ngono ili kulinda kibarua”amesema Mussa

Kwa upande wake Mratibu na Mkurugenzi wa Sauti ya Jamii Kipunguni Bishagazi amesema semina hiyo ni muendelezo wa kampeni ya kuzuia rushwa ya ngono kwa wasichana wa kazi za ndani ili waweze kuvunja ukimya wa masuala hayo na kuwawezesha kuripoti vitendo hivyo kwenye mamlaka husika