May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanawake waaswa kupima afya zao kujitambua

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Mhe.Riziki Pembe Juma amesema upimaji wa afya ni muhimu sana kwa wanamke na mtoto, kwani uchunguzi husaidia kutathmini hali ya afya na kusaidia kutambua matatizo yoyote yanayoweza kutokea.

Pia amesema hatua hiyo itawasaidia katika kuwakinga watoto na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia.

Mhe Riziki ameyasema hayo kwa niaba ya Mwenyekiti wa Taasisi ya Maisha bora Foundation mama Maryam Mwinyi, katika kampeni ya Afya bora maisha bora iliyofanyika katika viwanja vya Kivunge Wilaya ya Kaskazini A Unguja.

Amesema Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto imefanikiwa kuweka namba ya simu inayotambulika 116 kwa kupiga bure, ikiwa lengo ni kutoa taarifa masuala yote ya udhalilishaji na kuweza kufuatiliwa na kuchukuliwa hatua.

Ametoa wito kwa wazazi na walezi kuwasaidia watoto wanapowapatia taarifa za vitendo hivyo, huku akiwasihi kurejesha malezi ya pamoja ili kuwakinga watoto juu ya vitendo hivyo.

Aidha kwa upande wake binafsi Mhe.Riziki ameipongeza Taasisi ya Maisha bora Foundation kwa ushirikiano mkubwa wanaoutoa kwa Serikali katika kupiga vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia hapa nchini.