May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanahabari, wafungwa washerekea kwa pamoja siku ya wanawake duniani

Judith Ferdinand, Timesmajira Online

Waandishi wa Habari Wanawake ambao ni wanachama wa Klabu Waandishi Mkoa wa Mwanza ( MPC ) wamewatembelea wafungwa wanawake wa Gereza Kuu la Butimba katika kusherekea siku ya wanawake duniani Machi 8,2024 pamoja na kuwapa zawadi mbalimbali.

Miongoni mwa vitu walivyotoa ni pamoja na nguo za ndani za wanawake,sabuni za miche na unga,taulo za kike pamoja na nguo za watoto zoezi lililoenda sambamba na upandaji wa miche ya miti ya matunda 100 iliyotolewa na Wakala wa Misitu Tanzania(TFS) Kanda ya Ziwa kupitia ofisi yake ya Wilaya ya Nyamagana.

Akizungumza mara baada ya kutoa zawadi hizo Makamu Mwenyekiti wa MPC Debora Mallaba,amewapongeza waandishi wa habari wanawake Mkoa wa Mwanza kwa kujitolea pamoja na uongozi wa Gereza hilo kwa kukubali wao kuwatembelea wafungwa hao.

Pia ameishukuru TFS kwa kuwapatia miche hiyo 100 ambayo wameipanda katika eneo la gereza hilo kwani anaamini baada ya miaka kadha itaadha kutoa matunda ambayo watatumia wafungwa waliopo gerezani hapo.

“Kwa uwezeshaji wa TFS tumepanda miche 40 ya parachichi,40 ya michenza na 20 ya machungwa,”ameeleza Mallaba.

Kaimu Mkuu wa Gereza Kuu la Butimba Lugalo Msomba amewashukuru na kuwapongeza waandishi wa habari wanawake kwa kutambua uwepo wa wanawake katika gereza hilo.

“Mwenyezi Mungu awabariki pale mlipotoa mkaongezewe,mliokuwa mnaweza kupeleka msaada sehemu nyingi ila mkaamua kuja hapa,msiishie leo tu mje na wakati mwingine,”.

Naye Mrakibu wa Magereza SP Mariam Lumuli , ameeleza kuwa serikali inajitahidi kwa kiasi kikubwa kuwahudumia wafungwa hao lakini kulingana na wingi wao haiwezi kutosheleza hivyo wadau ni watu muhimu .