March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanachama TAPIE watangaziwa mikopo yenye masharti nafuu

Na Mwandishi Wetu

BENKI ya CRDB imeahidi kuwapa mikopo yenye masharti nafuu na riba ndogo wamiliki wa shule binafsi ambao ni wanachama wa Chama cha Wawekezaji Binafsi katika Elimu (TAPIE).

Ahadi hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, wakati akifungua mkutano mkuu wa tatu wa TAPIE Mbezi jijini Dar es Salaam, ambapo yeye alikuwa mgeni rasmi.

Nsekela ametoa ahadi hiyo baada ya kusikia kilio cha wanachama wa chama hicho kuhusu ugumu wnaoupata kupata mikopo na ombi lao la kupungiziwa riba wanapopata mikopo hiyo.

“Ila kutakuwa na masharti madogo na nafuu kama vile mwenye shule kufungua akaunti CRDB na wanafunzi wenu wote kufungua akaunti kwetu maana hawo ni wateja wetu wa baadaye,” amesema Nsekela.

Amewataka wamiliki wa shule binafsi nchini kuwafundisha elimu ya kutunza fedha wanafunzi tangu wakiwa wadogo ili waje kuwa wajasiriamali wakubwa na mahiri wanapomaliza masomo yao ya elimu ya juu.

“Huwezi kuwa mjasiriamali mzuri kama hujui kutunza fedha, sasa wafundisheni umuhimu wa kutunza fedha na wafungulieni akaunti hii itawajengea utamaduni mzuri wakiwa wakubwa ,” amesema Abdulumajid

Pia amepongeza shule binafsi kwa kuendelea kufanya vizuri kitaaluma na aliipongeza pia serikali akisema kuwa kufanya vizuri kwa sekta binafsi katika elimu ni matokeo ya jitihada za serikali kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji wa sekta hiyo.

Amesema kufanya vizuri kwa shule nyingi binafsi kumewavutia wazazi wengi kuwapeleka watoto wao kwenye shule hizo hata pale wanapofaulu kujiunga na shule mbalimbali za umma.

Amesema kwa kutambua umuhimu wa elimu benki ya CRDB imeiweka sekta ya elimu kama sekta ya kipaumbele kwa kuendelea kuiwezesha kwa mikopo na mitaji.

Nsekela amesema mwaka jana na nusu ya mwaka huu shule nyingi zilipata shida kutokana na janga la COVID 19 lakini benki hiyo iliweka mazingira rafiki kwa kuhakikisha wenye shule wanapewa muda mwingi wa kulipa mikopo.

Mkurugenzi Mkuu wa benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, akiwa kwenye picha ya pamoja na wafanyakazi wa benki ya CRDB Mkutano wa Mwaka wa Chama cha Wamiliki wa Shule Binafsi (TAPIE), uliofanyika jana jijini Dar es Salaam. Mwenye suti ya kahawia kulia ni Mkurugenzi wa shule za Tusiime, Dkt. Albert Katagira. Na mpiga picha wetu

“Shule nyingi zilikuwa kwenye mapumziko kutokana na janga hilo hivyo hali ya uchumi haikuwa nzuri kwao lakini sisi tuliwapitia mmoja baada ya mwingine kuangalia changamoto yake na kutafuta suluhu,” amesema

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TAPIE, Mahmoud Mringo aliomba benki mbalimbali zipunguze riba ya mikopo ili kuwawezesha wamiliki wa shule kupata mikopo nafuu.

Amesema uwekezaji kwenye elimu unachukua muda mrefu kurejesha faida lakini wamekuwa wakipata vikwazo sana kwenye kupata mikopo ikiwemo viwango vikubwa vya riba.

Amesema shule binafsi zimekuwa zikitozwa tozo mbalimbali za serikali hivyo kuwa na mzigo mkubwa wa kujiendesha hali inayowafanya wenye shule wengi kuishi wakiwa na msongo wa mawazo.