May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Walimu watakiwa kujiendeleza na mikopo nafuu

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online Arusha.

WALIMU wametakiwa kuwekeza na kujiendeleza katika mikopo nafuu yenye tija, yakuweza kutatua changamoto zinazowakabili ili kuweza kunufaika na kufurahia kazi wanazozifanya.

Akizungumzia hilo, Mwakilishi wa Mkuu wa mkoa wa Arusha,John Mongella katika mafunzo ya walimu mkoani hapo, yaliyoandaliwa na Benki ya NMB, Afisa elimu sekondari Khalifani Omary amesema, mafunzo hayo yatawajenga walimu katika kujiwekea kipato ili kujiendeleza kimaisha.

“Mafunzo haya yatawasaidia katika kuwaongezea elimu na kutoa fursa ya maoni namna wanavyoweza kunufaika na benki ya NMB, ikiwa jitihada hizi zitaleta matokeo chanya nakuleta faraja kwa jamii,”amesema Omary.

Afisa elimu huyo amesema, jitihada hizo ni nzuri na zinaunga mkono juhudi za serikali katika kuhakikisha watanzania waliowengi wanajumuhishwa katika mfumo rasmi wa kifedha ili kuinua vipato vyao na kiuchumi kwa ujumla, hivyo anatoa rahi kwa taasisi nyingine za kifedha nchini kufanya jitihada hizo kama NMB.

Aidha amsema, anashukuru huduma za kibenki zimeboreshwa na kusogezwa karibu na wateja wake kwani hapo awali walimu walipata taabu kutembea umbali mrefu, hivyo benki ya NMB imekuwa chachu ya maendeleo katika jamii kwa kuwanufaika wateja wake.

Kwa upande wake Mkuu wa biashara za Kadi wa benki ya NMB, Philbert Casmir amesema wameandaa mafunzo yanayoitwa siku ya walimu ambapo wameanza mkoani Arusha kwa kutambua mchango wa mwalimu katika jamii na kutoa suluhisho ya changamoto zao katika kujikwamua kimaisha ikiwemo mikopo nafuu na bima mbalimbali.

“Tunatambua mwalimu ni mwezeshaji katika jamii, hivyo NMB tumekuja na muundo wa kutokutoa bidhaa au suluhisho ya maisha ya walimu, kwani tunatambua kunachangamoto za ujenzi na kupitia mafunzo haya, wataelimishwa nakuweza kutumia mikopo nafuu ya NMB kujiendeleza katika swala la ujenzi wa nyumba,”amesema Mkuu huyo.

Casmir amesema, kuna bima za walimu na watanzania kwa ujumla zinazoweza kuwasaidia kupata fedha, pamoja na hilo pia kunachangamoto ya elimu ya fedha watu kutoweka katika taasisi za kibenki na kutunza majumbani, hivyo elimu hiyo itawasaidia kufikisha ujumbe na faida za kuweka fedha benki katika jamii.

Hata hivyo baadhi ya walimu hao wamesema, wanaishukuru benki ya NMB kwa kuwapa mafunzo hayo ambayo yatawasaidia katika kuwekeza fedha na kutumia katika matumizi sahihi ya kujiendeleza kiuchumi na kuwaletea maendeleo.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Daraja mbili , Zukra Kalunde amesema mafunzo hayo yatawasaidia katika kufahamu umuhimu wa kadi pamoja na kujifunza namna ya kupata mikopo nafuu ya benki hiyo, itakayowasadia kujiendeleza kiuchumi kama ujenzi wa nyumba zao za kuishi na biashara.