May 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waandishi wa Habari watakiwa kujikita zaidi katika kuelimisha juu ya uhalifu

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Imeelezwa kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa katika kuibua,kupambana na kuzuia uhalifu,hivyo wito umetolewa kwa waandishi wa habari kuripoti habari zinazoelimisha jamii zaidi kuliko kuripoti matukio ya uhalifu.

Hayo yameelezwa na Kamishina wa Fedha na Uchumi wa Jeshi la Polisi nchini Hamad Khamis Hamad wakati akifungua mkutano uliofanyika kwa njia ya mtandao ulioandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari wa kupiga vita matumizi ya Dawa za kulevya na uhalifu Tanzania(OJADACT) kwa kushirikiana na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) pamoja na Jeshi la Polisi Nchini.

Kamishina Hamad,ameeleza kuwa,ukusanyaji na usambazaji wa taarifaa za uhalifu ziwe kwa maslahi ya umma na zitoke katika vyanzo sahihi vya jeshi la polisi na kuzingatia misingi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.

Amesema,suala la ushirikiano kati ya jeshi hilo na waandishi wa habari liwe la mkakati na ukusanyaji na usambazaji wa taarifa za uhalifu ziwe zenye lengo la kubadilisha mitazamo ya jamii katika vitendo vya uhalifu hasa vijana.

“Lazima kuwe na mkakati wa pamoja baina ya jeshi la polisi na vyombo vya habari ili kuzuia uhalifu nchini,vyombo vya habari vina nguvu na uharaka wa kuifikia jamii na endapo vikitumika katika kutoa taarifa za elimu juu ya uhalifu vitasaidia sana katika kuzuia uhalifu nchini,”amesema Hamad.

Msemaji wa Jeshi la Polisi David Misime,ameeleza kuwa

waandishi wa habari wajikite zaidi katika kuandika habari zinazohusu elimu ya athari za uhalifu kuliko kuripoti matukio.

Hivyo waandishi wanapaswa kuripoti habari zenye kueleweka bila kuleta taharuki kwa jamii na kutoa athiri ushaidi wa kesi pamoja na kuhakikisha kuwa taarifa za uhalifu kabla ya kuzitumia jeshi la polisi nalo limeshirikishwa itasaidia kulinda amani na usalama wa taifa

“Gharama za kupambana na uhalifu ni kubwa kuliko za kuibua na kuzuia, waandishi tumueni kalamu zenu katika kupambana na kuzuia uhalifu, tusiendelee na mtindo uliopo wa kuripoti matukio zaidi kuliko kutoa elimu zaidi ya namna ya kuelimisha watu kuchukia uhalifu,”amesema Misime

Kwa upande wake Mratibu wa THRDC Onesmo Orengurumwa, amesema matukio ya kihalifu yanayoendelea hapa nchini yanavunja haki za binadamu kwani hakuna takwa la kisheria la kutenda uhalifu,hivyo Jeshi la Polisi lifanye kazi kwa ukaribu na waandishi wa habari na watetezi wa haki za binadamu kwenye kupambana na uhalifu.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Habari,Wizara ya Mambo ya Ndani Christina Mwangosi,ameeleza kuwa kuripotiwa kwa matukio ya uhalifu kwa mfumo wa mfululizo au muendelezo (series) ni tatizo kubwa kwani yanaharibu upelelezi wa kipolisi na pia kuleta chuki kwenye jamii jambo ambalo halina tija pia inaweza kuvutia mtu kufanya uhalifu.

Mwenyekiti wa OJADACT Edwin Soko,amesema kuwa, vyombo vya habari viepuke kuripoti zaidi matukio na badala yake vijikite katika kuelimisha jamii juu ya uhalifu.

Kamishina wa Fedha na Uchumi wa Jeshi la Polisi nchini Hamad Khamis Hamad, akizungumza wakati akifungua mkutano uliofanyika kwa njia ya mtandao, ilioandaliwa na OJADACT kwa kushirikiana na THRDC pamoja na Jeshi la Polisi.(Picha na Judith Ferdinand)