April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waandishi wa habari endeleni kuzalisha habari za watu wenye ulemavu

Na Esther Macha,Timesmajira,Online,Dodoma

WAANDISHI wa habari nchini wametakiwa kuendelea  kuzalisha habari zenye tija katika jamii zinazohusu  watu wenye ulemavu kwa kuzingatia taalum na  miongozo ili kuhakikisha masuala ya walemavu  yanasikika ndani ya nchi na nje ya mipaka ya Tanzania .

Hayo yamesemwa leo na ofisa ustawi wa jamii mwandamizi kutoka ofisi ya waziri mkuu anayeshughulikia masuala ya watu wenye ulemavu ,Joyce Maongezi wakati wa kongamano la kimataifa la siku ya walemavu duniani ambayo imefanyika mkoani Dodoma  ambalo limehusisha taasisi mbalimbali zinazofanya kazi na watu wenye ulemavu  kutoka Tanzania bara na Zanzibar pamoja na waandishi wa habari.

Maongezi amesema kutokana na mchango mkubwa wa waandishi wa habari katika kuhabarisha jamii kuhusu masuala ya watu wenye ulemavu serikali ina imani kubwa kuwa waandishi wa habari watatumia vema kalamu zao kuhabarisha jamii kuhusu masuala ya  walemavu ili yaweze kusikika kote nchini na hata nje ya mipaka ya nchi.

“Serikali tumefurahishwa sana na shirika la Internews Tanzania  kwa kazi kubwa wanayofanya kuwawezesha waandishi wa habari kwa kuwapatia rasilimali fedha ili waweze kuibua habari za watu wenye ulemavu na hatimaye kusikika kote nchini  Tanzania na hata nje ya mipaka ya nchi yetu”amesema Maongezi.

Akifungua kongamano hilo leo Mratibu wa shirika la  Internews Tanzania ,Shaban Maganga amesema kuwa lengo la kongamano hilo ni kuwapa fursa  waandishi wa habari na wadau kujadili kwa pamoja ikiwa ni  sehemu ya maadhimisho ya siku  ya kimataifa ya  watu wenye ulemavu.

Akielezea zaidi Maganga amesema kuwa mtu yeyote anaweza kuwa mlemavu wakati wowote na kwamba  kuwa mlemavu  sio kwamba inaaminisha kuwa huwezi kufanya shughuli yeyote hivyo Internews imewakutanisha wadau ili kukumbusha mambo muhimu kupitia majadiliano.

Mkurugezi mtendaji wa shirika la youth with Disabilities (yowdo)Rajabu Mpilipili ameshauri taasisi mbalimbali ikiwemo serikali na watu binafsi kuendelea kuelimishwa juu ya kuwahusisha watu wenye ulemavu  katika masuala ya kijamii ikiwa ni pamoja na ajira.

“Tuna walemavu wengi ambao ni wasomi tunaomba waonwe katika taasisi hizo tunaamini katika kundi hili tuna watu wenye uwezo mkubwa na wana vigezo “amesema Mpilipili.

Kwa upande wake Mwazilishi na Mkurugenzi mtendaji wa shirika la Lukiza Autism  foundation aliomba jamii  kuweka mkazo  umuhimu  wa kuzingatia watu wenye ulemavu  wa akili na mfumo wa fahamu na usonji kwa kuwa aina  hiyo ya ulemavu ipo na imekuwa ikiongozeka kadri siku zinavyoenda.