April 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vyombo vya habari vyatakiwa kurusha habari za hali ya hewa

Na Penina Malundo,Timesmajira Online

NAIBU Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Tulia Ackson (MB), ametoa wito kwa vyombo vya habari kutenga muda wa kutosha wa kurusha taarifa za hali ya hewa mara kwa mara kwa lengo la kusaidia wananchi kuzipata taarifa hizo kwa wakati na kuzitumia kwa ufanisi zaidi.

Akizungumza hayo leo, mkoani Dar es Salaam wakati alipotembelea Makao Makuu ya Mamlaka hiyo, Dkt. Tulia amesema kutokana na muda wa habari ya hali ya hewa kuwa mfupi na taarifa zinatolewa kwa ujumla zinakuwa jamb ambalo linaweza kuathiri matumizi yake.

“Nitoe wito kwa vyombo vya habari kuangalia namna ambavyo watakuwa wanazitumia taarifa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na kuzitoa mara kwa mara ili kutusaidia sisi wananchi kujiandaa na kufanya maamuzi sahihi katika mipango yetu, tuangalie kama vyombo vingine vya habari vya mataifa ya nje, ukifungua kila wakati unaangalia hali ya hewa,”ameaema Dkt. Tulia.
Amesema, alichojifunza katika ziara yake fupi katika ofisi za Mamlaka hiyo ni kuwa taarifa za hali ya hewa zipo, lakini kwa ajili ya muda mfupi Mamlaka inalazimika kuziweka katika huo muda mfupi.

Aidha Dkt. Tulia ametoa wito kwa wananchi kuitembelea Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ili kujifunza masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na namna taarifa za hali ya hewa zinavyochakatwa kitaalamu hadi kumfikia mtumiaji.