April 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waandishi wa Habari wakiwa kazini, (Picha ya Maktaba)

Vita ya Corona yatua kwa wanahabari nchini

Na Waandishi Wetu, Dadoma, Zanzibar

KUANZIA leo vyombo vya habari nchini vinatakiwa kuwa na mwandishi mmoja kwa ajili kuripoti habari za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaloendelea jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya hatua za kukabiliana na maambukizi ya Corona.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na mmoja wa maofisa wa Idara ya Habari Maelezo utekelezaji wa maamuzi hayo unaanza leo.

Wakati huo huo Wizara ya Habari, Utali na Mambo ya Kale imetoa mwongozi wa utoaji habari kwa wananchi ambapo kuanzia sasa mikutano ya waandishi wa habari na shughuli nyingine zitakazowafanya waandishi wa habari kukusanyika zimesitishwa.

Hiyo ni kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na Mkurugenzi Idara ya Habari (MAELEZO) Zanzibar, Dkt. Jurna Mohammed Salum. Hatua hiyo imekuja kufuatia idadi ya wagonjwa wa Corona kuwa imeongezeka visiwani humo, ambapo jana wamethibitika wagonjwa wapya watatu.

“Taarifa za Waziri wa Afya Zanzibar kuhusiana na Virusi vya ugonjwa wa Corona zitatolewa kwa njia ya ‘Press Releases’, kurusha moja kwa moja kupitia Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) au kurekodiwa na kusambaza taarifa hiyo kwa vyombo vya habari na umma kwa ujumla,” ilieleza taarifa hiyo na kuongeza;

“Taasisi zote zenye shughuli zitakazowajumuisha waandishi wa habari tunawaomba kutumia njia tulizozieleza na kujiepusha kwa namna yoyote ile kuwaita waandishi wa habari katika shughuli zao.”

Kupitia taarifa hiyo wahariri na waandishi wa habari wamesisitizwa kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya na Serikali kwa ujumla kwa kuepuka mikusanyiko.