April 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vinara wa mitindo kukutana Safari fashion Weekend

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

MANGULI wa mitindo nchini wanatarajiwa kushiriki tamasha la mavazi liitwalo Safari Fashion Weekend litakalofanyika Januari 28 hadi 30 mwaka huu katika Hoteli ya Mawemawe mkoani Manyara.

Wabunifu hao ambao tayari wamethibitisha kushiriki katika tamasha hilo ni Ally Rehmtullah, Bahati Zanzibar, Cocolili, Doreen Mashika, Jamilla Vera Swai, Martini Kadinda, Mustafa Hasanali na Schwari.

Lengo la tamasha hilo ni kukuza na kutangaza utalii wa ndani kupitia tasnia ya mitindo pia kuonyesha mavazi yanayo valiwa katika safari za utalii.

Kabla ya tamasha hilo ambao kiingilio kutakuwa ni dola 50 kutakuwa na shughuli za utalii wa ndani ambapo wabunifu watatembelea vivutio vilivyomo ndani ya Hoteli ya Mawe Mawe.

Januari 29 kutakuwa na mnada ambao wabunifu watauza mavazi yao na bidhaa zengine Mawemawe hoteli.

Usahili kwa ajili ya kupata wanamitindo watakaoshiriki tamasha hilo utafanyika Januari 15, mwaka huu katika Ukumbi wa Makuti Restaurant uliopo Oysterbay jijini Dar es Salaam.