May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vijana wavivu washukiwa

Na Queen Lema, Timesmajira Online,Arusha

Askofu Mkuu wa makanisa ya Pentekoste Revival Church, Lwaga Njeni amewataka vijana nchini hapa kuhakikisha kuwa wanapata fedha pamoja na utajiri kwa njia ambayo ni ya halali na kuacha kupita njia za mikato.

Kwa sasa vijana wengi ni wavivu hivyo wamebuni njia ambazo wanajihusisha na imani ambazo sio za kweli na wanafanya hivyo ili waweze kujipatia fedha.

Askofu huyo ameyasema hayo siku chache zilizopita wakati akiongea na watanzania kupitia kongamano ambalo limefanyika kwenye kanisa la Pentekoste Revival Church Mbauda jijini Arusha.

Ambapo amefafanua kuwa njia za mikato hasa za kujipatia fedha sio salama badala yake kinachohitajika ni uwajibikaji katika nyanja mbalimbali.

“Katika imani wapo baadhi ya vijana hasa hawa wenye imani wanasahau imani ya kikristo wanajikuta wakiwa wanadanganya watu kwa kununua vitu mbalimbali ambavyo wanadai kuwa ni muujiza,”amesema Askofu Njemi.

Wakati huo huo amewataka wazazi kuhakikisha wanawasomesha watoto wao ili kuondokana na adui mbaya ambaye ni tamaa.

“Wazazi hakikisheni kuwa mnawasaidia vyema watoto wenu kupata elimu zote zinazohitajika katika maisha yao,unapowasomesha inaweza kuwasaidia kuepukana na adui mbaya sana tamaa, lakini pia hata udanganyifu,”amesisitiza.

Hata hivyo amewataka wakazi wa Arusha kuchukua tahadhari dhidi ya matapeli wa injili ambao wanarahisiha maisha kwa njia ya utapeli.

Naye Mama Askofu wa kanisa hilo Wodie Njeni amesema kuwa ili vijana na taifa liweze kwenda mbele katika mafanikio ni lazima wahakikishe wanaachana na tabia ya uvivu.

“Uvivu ni dhambi kubwa sana na ni dhambi ambayo inatakiwa kupingwa kwa hali ya juu sana niwaambie tu kuwa uvivu ni dhambi kubwa sana,”.