April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

UVCCM yamkingia kifua Rais Samia Urais CCM 2025

Na Mwandishi Wetu, TimesmajieaOnline,Iringa

JUMUIYA ya Umoja wa Vijana (UVCCM) imesema itawashughulikia watakaojitokeza ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuchukua fomu kugombea nafasi ya urais katika Uchaguzi Mkuu 2025.

Jumuiya hiyo imewaomba wana CCM kumuachia Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, awe mgombea pekee atakayepeperusha bendera ya CCM ngazi ya urais katika uchaguzi huo.

Akizungumza na wananchi wilayani Kilolo mkoani Iringa katika mkutano wa hadhara wa uzinduzi wa kampeni ya Jiandikishe, Chagua CCM uliofanyika kata ya Nyalumbu, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Muhsin Ussi, alisema.

“Kutokana na kazi na kasi kubwa ya maendeleo inayofanywa na Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi Dkt. Samia, hakuna sababu ya mwa CCM kujitokeza kuchukua fomu ya kugombea urais.”

Amesema katika nafasi ya Rais, Vijana wa UVCCM wameweka msimamo wao kuwa fomu itakayotoka ni moja ambayo atachukuliwa Dkt.Samia, hii inatokana na kazi kubwa aliyoifanya katika kipindi kifupicha miaka mitatu.

Alisema atakayethubutu kuchukua fomu ataiona rangi ya umoja wa vijana wa CCM unaoongozwa na Mwenyekiti, Mohamed Kawaida.

Akimkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Iringa, Agrey Tonga, alieleza kuwa vijana wote wenye sifa na vigezo wajitokeze kwa wingi kuchukua fomu kugombea katika uchaguzi wa Serikali za mitaa.

Toga amesema UVCCM itawaunga mkono vijana wote watakaogombea katika uchaguzi huo na uchaguzi wa Serikali za mitaa ili kujenga uwakilishi wa vijana katika maamuzi ya Taifa na kuleta maendeleo endelevu.

Naye Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Kilolo, Amani Mdeka, alisema kuwa UVCCM imejipanga kuhakikisha katika uchaguzi wa Serikali za mitaa unaotarajia kufanyika mwaka huu chama cha Mapinduzi CCM kinashinda kwa kishindo mitaa yote.