March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Utafiti:Magonjwa yasiyo ya kuambukiza,majeruhi yashika Kasi kwa asilimia 41

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

RIPOTI ya Mwaka  2020 ya Takwimu za Kamisheni ya Umasikini na Magonjwa imeonyesha kuwa asilimia 41 ya utafiti uliofanyika Tanzania katika kipindi hicho ,ni  ya magonjwa yasiyoambukiza na majeruhi.

Aidha Utafiti huo umeonyesha kuwa mwaka 2020 Tanzania ilitumia dola milioni 700  kugharamia katika kukinga na kutibu magonjwa hayo.

Akizungumza katika mkutano wa kutoa ripoti ya matokeo ya utafiti katuika sekta ya afya uliofanywa na  watafiti mbalimbali hapa nchini, Profesa Goodluck Makundi alisema, magonjwa yasiyo ya kuambukiza hapa nchini bado ni changamoto.

“Kuna ongezeko la magonjwa yasiyoambukizwa nchini Tanzania na kufikia vifo,ongezeko hili ni mara mbili ya hali ilivyokuwepo mwaka 2015,hali hii inasababisha nguvu kuelekezwa zaidi katika  kutibu kuliko kukinga ,na ni ghali  kutibu kuliko kukinga.”

Profesa Makundi alisema tatizo  hilo haliwakumbi watu wazima na wazee tu bali hata vijana na watoto wanakumbwa huku akisema linachangiwa sana na  mabadiliko ya mtindo wa maisha na lishe .

Aidha alisema,hilo ni tatizo mtambuka linahusisha sekta mbalimbali.

“Ni changamoto kubwa hapa nchini kwa magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza ,magopnjwa haya ni pamoja na moyo,shinikizo la damu,saratani mbalimbali pamoja na magonjwa ya mfumo wa hewa.”alisema na kuongeza kuwa

Profesa Goodluck alitaja baadhi ya vitu vinavyosababisha magonjwa yasiyo ya kuambukiza kuwa ni pamoja na matumizi ya tumbaku,kutofanya mazoezi,ulaji vyakula usiozingatia lishe bora na matumizi ya  pombe kupita kiasi.

Alisema,Shirika la Afya Duniani linasema,mambo hayo yanachangia kwa asilimia 80 ya tatizo hilo duniani.

Akizungumzia kuhusu matokeo ya utafiti uliofanywa na watafiti katika sekta ya afya alisema,matatizo ya magonjwa hayo yasiyo ya kuambukizwa na majeruhi inachangia kwa asilimia 41 ya vifo na walemavu.

Vile vile alisema,matokeo ya utafiti wao umeonyesha,pamoja na mambo mengine kuna upungufu wa fedha za kugharamia magonjwa hayo ambapo asilimia 7.8 ya matumizi ya sekta hiyo ndio hutumika ikilinganisha na tatizo  la asilimia 41 .

Akitoa mapendekezo katika sekta ya afya alisema,inahitaji uratibu wa hali ya juu kwa kutumia ofisi mbalimbali ikiwemo Ofisi ya Rais Tamisemi,lakini pia sheria na kanuni zilizopo dhidi ya mapambano ya magonjwa yasiyo ya kuambukizwa ziimarishwe .

“Mfano bidhaa za mazao ya tumbaku ziongezwe  kodi pamoja na kupiga marufuku matangazo yake.”

Vile vile alisema pendekezo linguine ni kuanza kuzungumzia elimu ya magonjwa haya katika ngazi  tofauti tofauti,pia yaingizwe kwenye mpango wa elimu ya afya mashuleni.

Profesa Makundi pia alisema pendekezo linguine ni ,vyombo vya habari vikiwemo vya mitandao ya kijamii ,vilete  mabadiliko kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusiana na magonjwa hayo.

“Social media(mitandao ya kijamii) inaweza kutumika ‘positively’…,maana media ni eneo ambalo tukishirikiana vizuri linaweza kuleta matokeo chanya .”alisisitiza

Pia alisema watafiti katika eneo hilo la afya wamependekeza kuwepo na uwekezaji zaidi huku akisema,kuna haja ya kutafiti zaidi na kuwekeza kwenye utafiti ili kutatua matatizo hayo lakini pia kuna haja ya kutumia maafisa maendeleo ya jamii kuelimisha watu katika ngazi tofauti tofauti.

Katika hatua nyingine alisema viongozi wa dini pia wanao wajibu wa kuelezea angalau kwa dakika chache wawapo katika ibada zao huku akisema,hii itasaidia waumini kupata uelewa juu ya magonjwa haya katika maeneo tofauti tifauti a kuwapa uelewa wa kutosha.

“Kwa hiyo tunaona kuna haja ya kutumia majukwaa tofauti tofauti katika kupambana na magonjwa haya,lakini pia  kila  mtu ahusike katika kuchukua hatua ikiwemo kufanya mazoezi,pia taasisi mbalimbali zikiwemo shule shule nazo zina jukumu la kuhamasisha mazoezi..,pia vyakula vyakula nyumbani vizingatie suala la lishe .”alisisitiza Profgesa Makundi

Awali akifungua hafla hiyo iliyoandaliwa na Tume ya Sayansi ,Teknlojia na Ubunifu (COASTECH) mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa COASTECH Dkt.Wilbert  Manyilizu alisema, lengo la warsha  hiyo ni kuwashirikisha Wadau wakuu wa matokeo ya tafiti za kisayansi na  Teknolojia ili waweze kuwasilisha na kutoa matokeo ya tafiti zao.

Alisema,Coastech iliwaita watafiti katika Sekta nne za awali ambazo ni sekta ya Afya,Kilimo,maliasili na mifugo  ili wawasilishe tafiti zao ambazo hufanyiwa kazi na Tume hiyo ambayo ndio yenye dhamana ya kuishauri Serikali katika masuala ya sayansi na teknolojia.

Aidha alisema,lengo la kuanzishwa kwa Tume hiyo ni  kuishauri Serikali katika masuala ya sayanasi na Teknolojia na ubunifu huku akisema,jukumu kubwa la COASTECH ni kuratibu na kuhamasisha Mambo ya utafiti na ubunifu ambapo katika jukumu hilo pia kuna majukumu mengine.

Ameyataja majukumu hayo kuwa ni pamoja na kusimamaia Menejimenti ya maarifa yanayopatikana katika ubunifu na utafiti na baadae kusambaza kwa Wadau huku akisema, michakato yote ya kuwatambua na kuwawezeaha wabunifu ni jukumu lao.

Aidha alisema,jukumu linguine la Tume hiyo ni kuhabarisha Wanachi na Wadau mbalimbali kwa kukusanya na kusambaza taarifa za sayansi  na ubunifu wa wananchi pamoja na kusambaza vijarida.