March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

UNAIDS yapongeza jitihada za serikali kukabiliana na UKIMWI

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online, Dar

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Ukimwi (UNAIDS) limepongeza jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kupambana na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Mkurugenzi Mkazi wa UNAIDS nchini, Dkt. Leo Zekeng alipoagana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam baada ya kumaliza muda wake wa uwakilishi nchini.

Dkt. Zekeng amepongeza jitihada zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kukabiliana na maambukizi ya Ukimwi hasa katika eneo la utoaji wa elimu kwa jamiii, kuanzishwa kwa Sera ya kudhibiti Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI pamoja na mikakati mbalimbali ya kupambana na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.

“Nilipowasili Tanzania miaka mitano iliyopita takriban asilimia 62 ya Watanzania walikuwa wanafahamu hali ya afya zao hasa kwa ugonjwa wa UKIMWI, ila sasa nafurahi kuwa takribani asilimia 90 ya Watanzania wanafahamu hali ya afya zao, hili ni jambo kubwa sana katika jamii,” alisema Dkt. Zekeng.

Dkt. Zekeng amesema malengo ya UNAIDS ni kuhakikisha kuwa kufikia mwaka 2025 hakutakuwa na mtoto atakayezaliwa na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.

Akizungumza katika tukio hilo, Balozi Mulamula amempongeza Dkt. Zekeng kwa kazi nzuri ya kutoa elimu na kampeni dhidi ya Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI ambapo kupitia kampeni hizo maambukizi ya ugonjwa huo nchini yamepungua kwa kiasi kikubwa.

“Elimu kuhusu maambukizi ya Virusi vya UKIMWI imekuwa msaada mkubwa katika jamii yetu, tunawashukuru UNAIDS kwa misaada ya dawa hasa ARVs pamoja na kampeni mbalimbali za kuelimisha jamiii juu ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI ambapo hadi sasa jamii imepata uelewa wa kujikinga na ugonjwa huo na maambukizi yamepungua kwa kiasi kikubwa,” alisema Balozi Mulamula.

Balozi Mulamula ameongeza kuwa miaka ya nyuma kulikuwa na unyanyapaa mkubwa katika jamii zetu lakini kutokana na elimu kuhusu maambukizi ya virusi vya UKIMWI pamoja na kampeni mbalimbali ambazo zimekuwa zikitolewa na UNAIDS kwa umma zimesaidia kupunguza unyanyapaa na maambukizi ya virusi vya Ukimwi nchini.

Aidha, Waziri Mulamula amemsihi Dkt. Zekeng kuwa balozi mzuri wa Tanzania kokote aendako Duniani ambapo Dkt. Zekeng ameahidi kuwa balozi mzuri wa Tanzania na kusisitiza kuwa Tanzania ni nyumbani kwake hivyo wakati wote atakuwa balozi mzuri.