April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Halmashauri ya Jiji la Mwanza kukusanya damu unit 200-250 kwa mwezi kusaidia wenye uhitaji

Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Katika kuhakikisha damu salama kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu wenye uhitaji inapatikana,Halmashauri ya Jiji la Mwanza imelenga kukusanya unit 200 hadi 250 za damu ndani ya mwezi mmoja.

Hivyo ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kuchangia damu ili kuweza kuokoa maisha ya watu wenye uhitaji ikiwemo wajawazito.

Hayo yamebainishwa na Mganga Mkuu wa Jiji la Mwanza Dkt.Sebastian Pima,wakati akizindua kampeni ya uchangiaji damu upitia Grasa gulio ilioanza Mei 12 -15, inayofanyika jijini Mwanza ilioandaliwa na mjasiriamali na Meneja shughuli wa Kijiji Bar and Grill Judith Mzurikwao kwa kushirikiana na wadau wengine ikiwemo Movit.

Dkt.Pima amesema,ndani ya Jiji wanazo hospitali kubwa ikiwemo hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando ambayo inahudumia mikoa ya Kanda ya Kanda ya ziwa lakini na hospitali nyingi ambazo zinafanya huduma za dharura kwa wajawazito ambao wengi wao wanahitaji damu.

Amesema,wao ndani ya Jiji wanamalengo ya kukusanya uniti hizo za damu ili kuweza kusaidia hupatikanaji wa damu ya kutosha kwani mahitaji ya damu ni makubwa na zoezi hilo linaendelea kwa siku tatu ni vyema wananchi wajitokeze ili kuokoa maisha.

“Lakini wote tunafahamu kwamba vifo vinavyotokana na uzazi bado ni vingi lakini jambo kubwa linalosababisha vifo hivyo ni kutokwa kwa damu nyingi kabla, wakati au baada ya kujifungua,zoezi hili kwetu sisi ni zoezi muhimu na kubwa ambalo lengo lake ni kwenda kuokoa maisha,wananchi msiishie mbali bali jitokezeni kwa wingi na kukutana na wataalamu wa afya kwa ajili ya kuchangia damu,”amesema Dkt.Pima.

Kwa upande wake muaandaji wa kampeni hiyo mjasiriamali na Meneja shughuli wa Kijiji Bar and Grill Judith Mzurikwao, amesema katika Grasa gulio kitu kikubwa anachofanya ni kuhamasisha jamii kuchangia damu.

Amesema anafanya hivyo kwani kila mtu kuna wakati anaweza akawa na uhitaji wa damu,hivyo ametoa wito kwa jamii katika siku hizo tatu na siku zingine wajitokeze kwenda kuchangia damu na kuondoa hofu pamoja na kuachana na maneno ya mtaani juu ya mtazamo hasi juu ya uchangiaji wa damu.

“Kitu kilichonisukuma mpaka kuja na jambo hili ni kutokana na kumpoteza ndugu yangu ambaye alikuwa na uhitaji wa damu lakini changamoto ilikuwa uhaba wa damu na benki ya damu ilikuwa haina damu hivyo wakati wa harakati za kutafuta damu mpaka kumpata mtu anayestahili kuchangia tulimpoteza ndugu yetu,”amesema Judith.

Ofisa Uhamasishaji wa Uchangiaji Damu Kanda ya Ziwa Neema Alex, amesema angalau kwa Sasa jamii ina uelewa kuhusu uchangiaji wa damu.

“Tunaendelea kuhamasisha jamii iendelee kuchangia damu,hili ni zoezi la sisi site kwa sababu damu anayohitaji mwanadami inatoka kwa mwanadami mwingine,”amesema Neema.

Baadhi ya wachangia damu waliojitokeza katika zoezi hilo akiwemo Zacharia Masasi, ametoa wito kwa jamii kujitokeza kuchangia damu

Mganga Mkuu wa Jiji la Mwanza Dkt.Sebastian Pima, akizungumza wakati akizindua kampeni ya uchangiaji damu upitia Grasa gulio ilioanza Mei 12 -15, inayofanyika jijini Mwanza ilioandaliwa na mjasiriamali na Meneja shughuli wa Kijiji Bar and Grill Judith Mzurikwao. (Picha na Judith Ferdinand)
Mganga Mkuu wa Jiji la Mwanza Dkt.Sebastian Pima, akipata vipimo kabla ya kuchangia damu wakati akizindua kampeni ya uchangiaji damu upitia Grasa gulio ilioanza Mei 12 -15, inayofanyika jijini Mwanza ilioandaliwa na mjasiriamali na Meneja shughuli wa Kijiji Bar and Grill Judith Mzurikwao.(Picha na Judith Ferdinand)
Muaandaji wa kampeni ya uhamasishaji wa uchangiaji damu,Mjasiriamali na Meneja shughuli wa Kijiji Bar and Grill Judith Mzurikwao, akizungumza wakati wa uzinduzi wa zoezi hilo linaloendelea kufanyika jijini Mwanza.(Picha na Judith Ferdinand)