May 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ujenzi Daraja la J.P.Magufuli wafikia asilimia 42, Mhandisi Gabriel aridhishwa na kasi ya utekelezaji

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Mradi wa ujenzi wa daraja la J.P.Magufuli mkoani Mwanza umefikia asilimia 42 huku nguzo 12 kati ya 67 zimekamilika ambapo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel,ameridhishwa na kasi ya utekelezaji wake.

Akizungumza mara baada ya kutembelea na kukagua namna utekelezaji wa mradi huo unavyoendelea Mhandisi Gabriel amesema, kama walivyoona kazi inafanyika,daraja hilo linapaswa kuwa na jumla ya nguzo 67 lakini mpaka sasa nguzo 12 tayari zimesimama.

“Kuna kazi kubwa ambayo imekuwa ikifanyika kwenye daraja hili,kazi nzuri kikubwa nipongeze timu nzima ya Mkandarasi lakini pamoja na wasimamizi na Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi,kikubwa matumaini yetu ni kwamba mwezi Februari mwaka 2024,daraja hili litakamilika,” amesema Mhandisi Gabriel.

Ambayo litawarahisisha watu wanaotoka Rwanda, Burundi,Kenya,Uganda wanaopitia maeneo haya kuweza kupita katika daraja hilo Hivyo kurahisisha sana usafirishaji.

“Nazidi kuwapongeza wasimamizi sababu kazi inafanyika mchana na usiku mahali hapa,fedha zinaletwa kwa wakati,na mnafahanu daraja ili limetoka serikali ya awamu ya tano na sasa ni awamu ya sita na mtiririko wa fedha ni mzuri,matumaini makubwa kwamba Watanzania ndani ya siku chache zijazo mwaka 2024 eneo hili litafunguka ambapo ni kiungo kikubwa cha uchumi kati ya Mkoa wa Mwanza na mikoa jirani lakini kati ya nchi yetu kupitia Mwanza na nchi jirani,”amesema.

Pia amesema,wote wanafahamu kwamba ni mradi mkubwa wa bilioni 699, na kazi inaendelea urefu wa daraja ni Kilomita 3.2,kazi ipo vizuri amekuwa akipita mara kwa mara ili kujiridhisha na kazi nzuri inatofanywa na serikali ya awamu ya sita.

Sanjari na hayo alimshukuru Rais kwani miradi yote ya kimkakati katika Jiji la Mwanza imeendelea kuletwa,fedha zinakuja kwa wakati, usimamizi upo vizuri lengo ni kutaka kuhakikisha matakwa ya miradi hiyo yote kwa kadri ya thamani ya fedha na muda wa mradi unakamilika kwa wakati.

Kwa upande wake Mhandisi Mshauri wa mradi wa ujenzi wa daraja la J.P. Magufuli Mhandisi Abdulkarim Majuto,amesema, mpaka sasa ujenzi unaendelea vizuri ambapo kati ya nguzo 67 zinazotakiwa katika daraja hilo nguzo 12 zimeisha inuka hata watu wanaopitia kwenye Ferry ( kivuko),wanaweza kuziona.

Ambapo utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 42 na matarajio yao ni kufikia Februari 2024 uwe umekamilika na kwa kasi ya Mkandarasi alionayo ana uhakika utakamilika ndani ya muda huo.

“Ujenzi unaendelea vizuri kwa maana kuwa Mkandarasi analipwa kwa wakati,pia kwa sasa tumeboresha usalama wa wafanyakazi katika daraja hili tumefunga camera kwenye daraja la muda na tunahakikisha wafanyakazi wanapata vifaa ambavyo wanavaa wakati wa kazi,”amesema Mhandisi Majuto.

Mhandisi Mshauri wa mradi wa ujenzi wa daraja la J.P. Magufuli Mhandisi Abdulkarim Majuto(aliye nyoosha mkono) akimuonesha kitu Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel,mara baada ya Mkuu huyo wa Mkoa kutembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa daraja la JPM namna utekelezaji wake unavyoendelea. (Picha na Judith Ferdinand.)
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel wa kwanza kushoto akikagua ujenzi wa daraja la J.P.Magufuli wakati alipo fanya ziara ya tembelea na kukagua mradi huo namna utekelezaji wake unavyoendelea. (Picha na Judith Ferdinand.)
Moja ya nguzo kati ya 12 zilizokamilika katika mradi wa ujenzi wa daraja la J.P.Magufuli ambazo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel,amezishuhudia mara baada ya kutembelea na kukagua mradi huo kwa ajili ya kujionea utekelezaji wake. (Picha na Judith Ferdinand)
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel wa akizungumza wakati alipotembelea na kukagua ujenzi wa daraja la J.P.Magufuli ili kujionea namna utekelezaji wake unavyoendelea. (Picha na Judith Ferdinand.)