April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Uchaguzi vyama vya soka Dodoma waahirishwa

Na Nuru Mkupa, Dodoma

KUFUATIA kauli ya Serikali iliyotolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ya kuendelea kusimamisha shughuli za michezo kwa muda usiojulikana, chaguzi mbalimbali za vyama vya soka vya Wilaya hazitafanyika hadi pale hali itakapokuwa shwari.

Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dodoma, Hamisi Kisoy amesema kuwa, chaguzi hizo mbalimbali za vyama vya soka vya Wilaya pamoja na washirika wao ndani ya Mkoa ambazo zilipangwa kufanyika mwezi huu.

Amesema, kutokana na janga lililozitesa ndhi nyingi duniani, wamelazimika kuzisogeza mbele hadi pale serikali itakapojiridhisha kuwa maambukizi yamemalizika.

Kisoy amesema kuwa, tayari chaka hicho kimeshaandika barua kwa vyama hivyo kuwaarifu kusitisha michakayo yote ya uchaguzi ambayo wengine walikuwa tayari wameshaanza maandalizi.

“Kwa sasa ni ngumu kuendelea na mchakato wa uchaguzi wa vyama vya Soka jijini hapa wakati hali halisi inaonekana, hadi sasa tumeshaandika barua kuviafiru vyama kusitisha michakato yote na tutaendelea nao pale Serikali itakapotangaza shughuli za michezo kuendelea kama kawaida,” amesema Kisoy.

Katika hatua nyingine, kiongozi huyo amewataka wachezaji kuendelea na mazoezi yao binafsi huku wakijilinda wakati wote kwani kwa sasa jambo muhimu zaidi ni kuchukua tahadhari ili wasipate maambukizi ya Corona.

“Tunaunga mkono Serikali kwa juhudi wanazochukua za kutoa elimu kwa wananchi hasa wanamichezo juu ya janga hili la corona na sisi viongozi wa michezo lazima tuchukue hatua ili kuwanusru wanasoka wetu,” ameweka wazi Kisoy.