March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TRA yajipanga kuwahudumia wananchi Sabasaba

Na Mwandishi wetu Timesmajira

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA)imesema imejipanga kikamilifu kuwahudumia wananchi wote watakaotembelea banda lao lililopo katika maonyesho ya 46 ya Biashara ya Kimataifa( DITF) yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julias Nyerere Jijini Dar es salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho hayo Mkurugenzi wa Huduma na Elimu ya mlipakodi, Richard Kayombo amesema miongoni mwa elimu watakayotoa ni pamoja na misamaha ya mlipa Kodi katika sekta mbalimbali.

“Wananchi wakifika katika banda letu watajua mabadiliko mbalimbali ya kodi yaliyotangazwa katika Bunge la bajeti la mwaka huu tunawaomba wawekezaji na wafanyabiashara wafike katika banda letu ili wapate elimu mahususi ya msamaha kwa walipa kodi”amesema Kayombo.

Pia Kayombo amewataka walipa kodi na wananchi kwa ujumla waendelee kuwaunga mkono TRA ili waweze kukusanya mapato kwa faida ya Taifa.

“Taifa linategemea ulipaji wa kodi wa wananchi ili liweze kufanya shughuli zake mbalimbali kwa ajili ya kuwahudumia wananchi”amesema

Aidha amesema katika maonyesho hayo kuna timu maalumu ipo kwa ajili ya kupokea maoni sambamba na uwepo wa huduma ya kujisajili kwa mtandao.