April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TFRA yatumia teknolojia kuwafikia wateja

Na Mwandishi wetu Timesmajira online

MAMLAKA ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) imesema imefanikiwa kusajili wafanyabiasha wa mbolea nchini zaidi ya 3800 kupitia mfumo wake wa kimtandao wa mbolea.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam katika Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya 46 yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julias Nyerere Jijini Dar es salaam, Kaimu Meneja Tehama na Takwimu TFRA Salehe Kejo amesema wafanyabiasha wengine 2200 wamesajiliwa kuanzia mwaka wa fedha 2022/23 kutika mfumo huo.

Amesema kuwa ongezeko la usajili wa wafanyabiashara limechangiwa zaidi na matumizi ya Tehama katika mamlaka hiyo.

Kejo ameongeza kuwa shughuli kubwa waliyoifanya katika Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) ni kuanzisha mfumo wa Kieletroniki au mfumo wa kimtandao wa mbolea uliorahisisha utoaji wa huduma kwa wateja.

“Wateja ambao waliokuwa wakitoka mikoa mbalimbali kuja Makao Makuu ya TFRA kufatilia Leseni zao, vibali ya kuingiza na kutoa mbolea sasa hivi wanapata huduma hizo kwa njia ya kimtandao.” Amesema Kejo.

Amesema Mfumo wa TFRA unamgusa moja kwa moja mteja kwani utoaji huduma umeimarika kutoka mteja kupata leseni kuanzia siku ya tatu hadi wiki, kwa sasa Mtu anapata Leseni ile ile ndani ya lisaa limoja tu.

Huduma nyingine zinazopatikana kwa haraka na kwa muda mchache ukilinganisha na muda wa kabla ya Mfumo wa kimtandao ni pamoja na vibali vya kuingiza na kutoa mbolea nchini na kusajili Mbolea.

Aidha ametoa wito kwa Wananchi kutembelea katika banda lao la TFRA ili waweze kupata elimu ya mbolea, matumizi sahihi ya mbolea .