April 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TMDA:Mipaka isiyo rasmi inakwamisha utendajikazi

Na Esther Macha, timesmajira,online,Mbeya

MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA),imesema kuwa,uwepo wa mwingiliano na nchi jirani umekuwa ukipelekea utekelezaji wa kazi mamlaka kuwa mgumu kutokana na uingizwaji wa bidhaa zisizosajiliwa kutoka nchi hizo za jirani.

Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa tiba,Anita Mshighati akionyesha baadhi ya bidhaa kwa waandishi wa habari jana.Picha na Esther Macha

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika viwanja vya Maonyesho ya Nanenane vya John Mwakangale Kaimu Meneja wa TMDA Nyanda za Juu kusini, Anita Mshighati amesema suala la mwingiliano na nchi jirani limekuwa na changamoto kubwa wakati wa kufanya ukaguzi kwenye mipaka.

Aidha Mshighati amesema kwamba mipaka isiyo rasmi imekuwa mingi hali ambayo imekuwa ikichangia uingizwaji wa bidhaa zisizosajiliwa.

“Miji iliyo karibu na mipaka imekuwa ikikutana na changamoto ya kuwa bidhaa ambazo hazijasajiliwa hivyo tumekuwa tukiendelea kukabiliana nalo kwa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa kushirikiana na halmashauri za wilaya ili nao waweze kujua namna ya kufanya kaguzi pale mamlaka inapokuwa mbali”amesema Mshighati.

Akizungumzia kuhusu ubora wa dawa kwa matumizi ya binadamu,Kaimu meneja huyo aliwataka wananchi kutumia dawa kulingana na maelekezo ya wataalam wanayopewa ili wasiweze kupata madhara.

Akielezea zaidi Mshighati amesema pia mamlaka imekuwa na majukumu ya kuchangia maendeleo ya nchi katika kuhakikisha wananchi wanakuwa na afya bora.

Kwa upande wake Mkazi wa Kigoe Wilayani Mbarali ,Bahati John alisema kitu kikubwa alichoweza kujifunza katika maonyesho hayo katika banda la mamlaka ya dawa na vifaa tiba ni pamoja na kutoa taarifa kwa dawa ambazo zimeisha muda wake,pamoja na kuwataka wananchi kutembelea banda hilo ili kuweza kujifunza zaidi.

“Leo hii nimetembelea mamlaka ya dawa na vifaa tiba nimejifunza vitu vingi sana ambavyo nilikuwa sivijui elimu hii nitapeleka kwa wenzangu nao waweze kujifunza zaidi hasa suala la dawa zilizoisha muda wake”amesema mwananchi huyo.