April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TGNP yatambua jitihada za Rais za kuhakikisha wanawake wanashika nafasi muhimu

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

MTANDAO wa Jinsia Tanzania(TGNP), umempogeza Rais Samia Suluhu Hassani kwa kuendelea kuzingatia jinsia katika uteuzi wa nafasi mbalimbali za uongozi .

Pongezi hizo zimetolewa baada Uteuzi uliofanyika juzi ambapo Dkt. Stergomena Tax ameteuliwa kuwa Waziri wa ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa huku Dkt Ashatu Kijaji akiteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.

Taarifa iliyotolewa na kwa Vyombo vya habari kwa niaba ya wanachama, Bodi ya wakurungezi, Wafanyakazi na watumishi wa Mtandao wa TGNP imeeleza kuwa TGNP imekuwa itambua jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha wanawake wanashika nafasi muhimu kwa mustakabali wa nchi .

“Nchi yetu imetengeneza historia kwani nafasi hizi kwa muda mrefu zimekuwa zikishikiriwa na wanaume kwa mara ya kwanza Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Ashatu Kachwamba Kijaji pamoja na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ambaye ni mwanamke na Dkt. Stergomena Tax, ambaye anakuwa mwanamke wa tatu kushika nafasi ya Uwaziri Ulinzi Afrika Mashariki”anaeleza.

Imeeleza kuwa hatua iliyofanyika ni kubwa sana katika historia ya harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi nchini na Afrika kwa ujumla.

Mkurungezi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Lilian Liundi

Taarifa hiyo imeeleza kuwa katika uteuzi wa Septemba 12 Rais Samia Suluhu Hassan aliweza kuteua viongozi watano mawaziri wanne (wanawake wawili na wanaume wawili) na hivyo, kufikia asilimia 50/50 ya uteuzi huo wa mawaziri.

Imebainisha kuwa pia Rais Samia Suluhu Hassan alimteua Mwanasheria Mkuu wa serikali ambaye ni mwanaume hivyo kwa ujumla Rais aliteua wanawake wawili sawa na asilimia 40 na wanaume watatu, sawa na asilimia 60.

Vilevile imeeleza kuwa uteuzi uliofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan umeongeza nafasi za wanawake mawaziri kufikia 7 sawa na asilimia 30.4 kutoka 5 sawa na asilimia 21.7 wakati huo wanaume wakiwa ni 16 sawa na asilimia 69.6 kutoka 18 sawa na asilimia 78.2 mwezi Marchi 2021 ambapo Rais Samia Suluhu Hassan aliposimikwa rasmi kama Rais wa awamu ya sita na kufanya mabadiliko madogo kwenye baraza la mawaziri lililoundwa na mtangulizi wake Rais John Pombe Magufuli.

Aidha walitoa wito kwa viongozi wanawake na wanaume walioteuliwa na Rais Samia kutumia nafasi na taaluma zao vyema kumsaidia kutimiza majukumu yake ya kuleta maendeleo endelevu na jumuishi nchini.