May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TFF waijia juu Simba

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

SHIRIKISHO la Soka nchini (TFF) limekeme vikali kauli iliyotolewa jana na Msemaji wa klabu ya Simba Haji Manara ya kuzuia mashabiki hasa wa klabu ya Yanga kuingia katika mchezo wao wa marudiano wa Ligi Mabingwa Afrika utakaochezwa Desemba 5 dhidi ya Plateau United ya Nigeria.

Jana wakati anatangaza viingilio kuelekea kwenye mchezo huo Manara alitoa angalizo kuwa hawataruhusu jezi isiyokuwa nyeupe na nyekundu kuingia katika mchezo huo kwani wanaposema hiyo ni mechi yao wanamaanisha.

Katika taarifa iliyotolewa leo na Ofisa Habari ya TFF, Cliford Ndimbo imesema kuwa, wanakemea vikali kauli hiyo kwani inalenga kuzuia haki ya mashabiki kuingia viwanjani.

Kwa mujibu wa Katiba ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu Ulimwenguni (FIFA) na ile ya TFF, vitendo vya aina yoyote ya ubaguzi havikubaliki katika mpira wa miguu hivyo shabiki yeyote anaruhusiwa kuingia kwenye mechi ikiwa tu havunji sheria na taratibu za soka ambazo zimeainishwa kupitia Katiba na kanuni husika.

Taarifa hiyo imeweka wazi kuwa, hata klabu ambazo zinamiliki viwanja hutenga tiketi maalum kwa ajili ya timu pinzani na makundi maalum.