April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TCB, FDT na Lonagro wazindua mikopo nafuu ya mashine za kuchana mbao

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira, Online, Mafinga

BENKI ya Biashara Tanzania (TCB) kwa kushirikiana na Taasisi ya Maendeleo ya Misitu Nchini (FDT) na Kampuni ya LonAgro Tanzania wameingia makubaliano ya kutoa mikopo nafuu ya mashine za kuchana mbao ili kuongeza uzalishaji wa mbao zenye ubora zaidi zitakazo weza kuingia kwenye ushidani katika soko la ndani na nje ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya hafla ya uzinduzi wa mradi wa mikopo nafuu wa mashine za kuchana mbao uliofanyika Wilayani Mufindi Mkaoni Iringa, Mkurugenzi wa Mikopo wa TCB, Henry Bwogi alisema mikopo hiyo inakusudia kukuza sekta ya misitu ili kuchangia zaidi katika pato la taifa na kuinua hali ya uchumi wa wananchi.

“Kumekuwa na changamoto kubwa katika upatikanaji wa mashine bora za kuchana mbao, hivyo tumetumia fursa hii kuongeza nguvu ili sekta ya misitu iweze kufanya vizuri na kuongeza mapato ya serikali sambamba na kuinua maisha ya mtu mmoja mmoja,” amesema Bwogi.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Maendeleo ya Misitu Nchini (FDT), David Shambwe(kushoto) wakipeana mikono na Mkurugenzi wa Mikopo wa Benki ya Biashara (TCB) Henry Bwogi (katikati) mara baada ya kusaini hati ya makubaliano ya kutoa mikopo nafuu ya mashine za kuchana mbao kwa wadau wa sekta ya misitu kwenye hafla iliyofanyika Mafinga juzi. Kulia ni Meneja kutoka Kampuni ya Lonagro Tanzania, Boniface Shayo.

Ameeleza kuwa makubaliano hayo yenye masharti nafuu yamewalenga wafanyabiashara na wajasiriamali katika sekta ya misitu hivyo ni wao kuchangamkia fursa hiyo ili waweze kuzalisha bidhaa bora zitakazokuwa na ushindani wa bei sokoni.

“TCB tunaamini katika ubunifu na kuleta bidhaa sokoni zitakazo wawezesha wananchi kutumia na kuwaletea faida kadhalika na kuongeza mapato kwa nchi yetu na kupelekea kufikia uchumi wa viwanda ifikapo 2025,” alisema Bw.Bwogi.

Amesema kumekuwa na matumizi ya teknolojia duni katika sekta ya misitu inayopelekea hasara kwa wafanyabiashara hivyo kupitia mikopo hii itawawezesha kupata mashine bora za kisasa ambazo zitawasaidia kuongeza uzalishaji wa mbao.

Mkurugenzi wa Mikopo wa Benki ya Biashara (TCB) Henry Bwogi (katikati) akiongea katika hafla ya uzinduzi wa mikopo nafuu ya mashine za kuchana mbao iliyofanyika Mafinga mkoani Iringa juzi. Kulia ni Meneja kutoka Kampuni ya Lonagro Tanzania wasambazaji wa mashine hizo,Bw.Boniface Shayo na kushoto ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Mufindi, Servi Ndumbaro

“Teknolojia inayokuwa ikitumika ni ya zakimani inayofanya zaidi ya asilimia 40 kupotea wakati wa kuzalisha mbao hivyo kupitia mashine za wood mizer kutoka kampuni ya Lonagro zitawezesha kuondoa upotevu huo,” alisema.

Aidha, Bwogi ameeleza kuwa vigezo na masharti ya kupata mkopo huo ni rahisi sana hivyo wanafanybiashara watembelee ofisi za benki hiyo zilizopo Mafinga na maeneo mengine ili wapatiwe maelekezo yatakayo wawezesha kupata mikopo hiyo.

Kwa upande wake Raisi wa Shirikisho la Viwanda vya Misitu Tanzania, Ben Mfungo Sulus aliishukuru benki ya TCB na FDT kwa kuleta mradi huo katika Wilaya ya Mufindi na kusema atawahamasisha wafanyabiashara katika sekta ya misitu kuchangamkia fursa hiyo ili kujipatia mashine zitakosaidia kurahisisha kazi na kuongeza ubora na thamani ya mbao.

“Niwaombe watoa huduma za mashine Lonagro Tanzania kuhakikisha mashine hizi zinapatikana kwa wakati pamoja na vipuli vyake kwa wafanyabiashara wamehamasika kutumia mashine hizi,” alisema Bw.Sulus.

Akifungua hafla hiyo Katibu Tawala wa Wilaya ya Mufindi, Servi Ndumbaro amesema hii ni fursa kwa wafanyabiashara za mbao katika kukuza biashara zao kupitia mkopo wa mashine kutoka TCB na kwamnba itasaidia kuongeza uzalishaji.

“wajasiriamali watumie fursa hii kukopa mashine hizi kupitia TCB ili waweze kunufaika katika biashara ya mbao aidha na kuiwezesha Wilaya yetu kupata mapato yatayosaidia kujenga miradi ya maendeleo,” amesema Ndumbaro,

Mikopo nafuu ya mashine za kuchana mbao inayotolewa na TCB umezinduliwa Wilayani Mafinga kama sehemu ya kuanzia na itaendelea katika maeneo mengine nchini. Pamoja na huduma hiyo TCB inatoa mikopo kwa wastaafu, mikopo ya vikundi na huduma nyingine.