May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tanzania,India zaungana kuadhimisha siku ya Makumbusho

Na Mwandishi wetu, Timesmajira online,Dar es Salaam

TANZANIA na India zaungana kuadhimisha siku ya Makumbusho Duniani huku zikisisitiza umuhimu wa uhifadhi wa urithi wa asili na utamaduni ambao utasaidia vizazi vya sasa na vijavyo kunufaika na urithi huo.

Akizungumza leo Jijini Dar es Salaam kwenye Maadhimisho hayo yaliyofanyika kwenye Kijiji cha Makumbusho, Naibu Balozi wa India,Mojar Varma amepongeza juhudi zinazofanywa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Makumbusho ya Taifa la Tanzania (NMT) kwa kazi nzuri ya uhifadhi wa urithi wa asili.

Varma amesema kuwa Tanzania na India zimekuwa na mahusiano mazuri na kushirikiana vyema katika nyanja mbalimbali hususan upande wa utamaduni.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa NMT, Dkt. Noel Lwoga alisema kuwa mwaka huu NMT imeadhimisha siku hiyo kwa kupanda miti, kutoa elimu, kufanya maonesho ya wajasiriamali pamoja na burudani ya ngoma za asili, muziki wa asili .

” Zoezi hili la kuadhimisha Siku hii pia katika vituo vingine vya Makumbusho nchini ambapo program mbalimbali za kielimu zimeendeshwa” amesema Dkt.Lwoga

Kufuatia hatua hiyo, Dkt. Lwoga ametoa wito kwa wananchi kuendelea kuzitembelea Makumbusho za Taifa ili kunufaika na elimu, burudani kupitia maonesho na mikusanyo iliyohifadhiwa na kuoneshwa kwenye matawi yote ya Makumbusho nchini.

Aidha, amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kupitia filamu ya Royal Tour na Wizara chini ya Mohammed Mchengerwa na Katibu Mkuu Dkt. Hassan Abbas kwa kuweka mikakati ya kuendeleza juhudi za kutangaza Utalii wa Makumbusho na Malikale.

“Kupitia juhudi hizo Makumbusho imeweza kupokea wageni zaidi ya milioni moja waka 2022”. amesema Dkt. Lwoga.