April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tamasha kubwa la injili kufanyika Mwanza, Kumuombea Rais Samia

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Filamu ya Tanzania “The Royal Tour”, iliyofanywa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, imeongeza idadi kubwa la watalii wanaokuja nchini Tanzania kwa ajili ya shughuli za utalii na uchumi wa Taifa umezidi kukua.

Hayo aliyasema jana Msanii wa Muziki wa Gospel, Rose Mhando wakati akitoa taarifa kuhusu tamasha kubwa la injili litakalofanyika jijini Mwanza katika uwanja wa CCM Kirumba Novemba 6, 2022 lenye lengo kumuombea Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan na kumkabidhi mikononi mwa Mungu ili aendelee kufanya kazi kubwa ambayo Mungu amempa ya kuongoza nchi na Taifa kwa ujumla na kumpa hongera kwa kazi kubwa aliyoifanya tangu alipoingia madarakani.

“Rais Samia amepambana kwa kufanya filamu ya Tanzania the royal tour na kufanya watalii wazidi kuongezeka Nchini, na East Afrika tumekuwa kwa kiwango kikubwa sana na hasa uchumi wa Taifa letu umekua sana” Alisema Mhando

Mhando alisema”Tunamuombea Rais kwasababu mimi kama mtanzania nimeona mambo makubwa sana ambayo Rais wangu ameyafanya katika Taifa langu la Tanzania , akiwa kama mwanamke shujaa, shupavu na hodari, amelibeba Taifa hili si kama Rais tu bali amelibeba kama mama akilibeba Taifa lote wakati wa Masika, kiangazi, adha na dhiki”

Mbali na hayo, Mhando alisema ameamua kuungana na wasanii wenzake kumuombea Rais Samia kwani wameona fursa nyingi ambazo zimepatikana kwa sasa kupitia yeye.

Aidha Mhando alisema Tamasha hilo halitofanyika Mwanza pekee, bali litafanyika katika mikoa mitano ikiwemo Dar es Salaam, Arusha na Mbeya.

Kwa upande wake Mratibu wa Tamasha hilo Emmanuel Mabisa alisema Maandalizi yote ya tamasha hilo yamekamilika , waimbaji wote ambao wametangazwa wako tayari kutumbuiza , wachungaji na maaskofu lakini pia mgeni rasmi watashiriki.

Mabisa alisema tamasha hilo litaanza saa2 asubuhi ambapo kiingilio ni elfu mbili kwa wakubwa na elfu moja kwa watoto.