April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tafiti zinaonesha kati ya Watanzania 100,tisa wana ugonjwa wa kisukari

Na. WAF – Mwanza

Tafiti zimebainisha kuwa kati ya Watanzania 100, watu Tisa wanaishi na Ugonjwa wa Kisukari kutokana na ongezeko la ugonjwa huo kila mwaka.

Hayo ameyasema jana Mwenyekiti wa Chama cha Kisukari Tanzania (TDA) Prof. Andrew Swai wakati akitoa mafunzo kwa wanafunzi wa Shule za Sekondari Jijini Mwanza.

Prof. Swai amesema wagonjwa wa Magonjwa yasiyoambukiza wanaongezeka kila Mwaka kutokana na mtindo mbaya wa maisha kwa kutozingatia vyakula pamoja na kutojishuhulisha na jambo lolote (Kazi au Mazoezi) hali inayopelekea kuwa na tabia bwete.

“Mazoezi ni muhimu sana angalau ufanye nusu saa kwa siku hii itasaidia utokwe na jasho ambalo hupunguza chumvi mwilini na kusaidia kutopata Magonjwa yasiyoambukiza kama Kisukari, Saratani na Presha, usikae siku nzima bila kufanya zoezi.” Amesema Prof. Swai

Aidha, Prof. Swai amewatahadharisha watanzania kupunguza kunywa vinywaji kama Soda, Juisi na Vilevi, hivi vyote hupelekea kupata Magonjwa hayo, akitolea mfano Soda kwa kawaida huwa na vijiko Tisa vya sukari.

Kwa upande wake Mkufunzi wa Mazoezi kutoka Shirikisho la Vyama vya Magonjwa Yasiyoambukiza Tanzania (NCDs Alliance) Dkt. Waziri Ndonde amesema Mtindo mbaya wa maisha ndio umetufikisha hapa hivyo tubadilike kwa kula vyakula halisi, kufanya mazoezi ili kupunguza unene, tuache kuwa na msongo wa mawazo na matumizi ya tumbaku.

Dkt. Ndonde amesema kuna mazoezi ya aina Tatu, ya Kwanza ni mwili unapotumia hewa ya Oxygen (Kukimbia na kutembea), Pili ni Kuimarisha misuli ya mwili (Kuvuta kamba, Kupiga Pushap), Tatu ni Kunyoosha viungo (Sarakasi, Kujikunja).

“Mazoezi yote haya yanatusaidia kufanya mwili kuwa imara, kujenga kinga ya mwili, kuwa na uzito ulio sahihi na kuepuka magonjwa haswa yasioambukiza.” Amesema Dkt. Ndonde.

Mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo wanafunzi hao na kwenda kutoa elimu hiyo waliyoipata kwa wengine lengo likiwa ni kudhibiti Magonjwa Yasiyoambukiza nchini.

Miongoni mwa wanafunzi wa Shule zilizopata mafunzo hayo ni pamoja na Pamba secondary, Mwanza secondary, Buhongwa secondary, Mugabe Girls selondari na Nsumba sekondari.