April 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Taasisi 150 kushiriki wiki ya azaki Dodoma


Na Zena Mohamed, Timesmajiraonline, Dodoma.

ILI kuonyesha mchango wa Asasi za Kiraia (AZAKI),katika maendeleo ya Taifa ,zaidi ya Taasisi 150 zitashikiriki katika maonyesho ya wiki ya AZAKI ambayo yatarajiwa kufunguliwa na spika wa Bunge la Tanzania Job Ndugai,kesho.

Hayo yamesemwa jijini hapa leo na Mkurugenzi mkazi, Nesia Mahenge wakati akiongea na vyombo vya Habari Kuhusu kuelekea wiki ya AZAKI ambapo amesema
itaanza na matembezi ya amani kuanzia saa moja asubuhi kutoka shule ya sekondari Dodoma hadi uwanja wa Jakaya Kikwete.

Mahenge ameeleza kuwa wiki hii inawaleta wadau mbalimbali wa Maendeleo nchini ikiwemo Wananchi,Serikali,AZAKI na sekta binafsi ambao wote Kwa Pamoja watajadili na kusherehekea mchango wa AZAKI katika kuleta maendeleo nchini.

“Tunawaita wadau mbalimbali wa maendeleo kujumuika nasi kwa ajili ya kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo ushauri wa kisheria,kufahamu kazi tunazofanya na kusherehekea kwa pamoja ,”amesema.

Pamoja na hayo Mahenge ameeleza kuwa uzinduzi huo wa wiki ya AZAKI utahudhuriwa na wahisani wa maendeleo wakiwemo ubalozi wa Denmark Utakaowakilishwa na Sascha Mulla na Ubalozi wa Canada utawakikishwa na Ms.Helen Fytche.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa United Nations Association (UNA) Reynald Maeda amewataja Viongozi na wageni mbalimbali kutoka Serikalini watakaoshiriki katika uzinduzi huo ni pamoja na Mkuu wa mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka,Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri,Meya wa Jiji la Dodoma Prof.Davis Mwamfupe na mwakili kutoka Wizara ya Afya Vickness Mayao.

“Katika kusherehekea mafanikio ya sekta ya AZAKI na ubia Wetu baina ya wananchi maonyesho yatakayofanyika tarehe 23 Hadi 24 Oktoba katika ukumbi wa Jakaya Kikwete na kutakuwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali kama Profesa Jay,Sheta,Barnabas,Gnako,na wasanii wa Dodoma,”amesema.

Ametaja faida ya kuwa na wiki ya AZAKI kuwa uwakutanisha wadau wa maendeleo kujadili masuala ya msingi kuhusu ustawi wa sekta pamoja na maendeleo ya Taifa Kwa ujumla.

“Maendeleo yanayoletwa na AZAKI si maendeleo ya kifedha tu bali Katika maeneo mengine ikiwemo maendeleo ya wananchi kupitia miradi mbalimbali ikiwemo kuongeza ushirikishwaji wa watu wote kwenye jamii,kupinga ukatili wa kijinsia Kwa wanawake na Watoto pamoja na kuongeza nguvu Katika ufuatikiaji wa rasilimali za umma,”amesema.