May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yazishukuru Ufaransa, Norway kuchangia miradi ya umeme vijijini

Na Veronica Simba, DSM

Serikali ya Tanzania imezishukuru nchi za Ufaransa na Norway kwa mchango wake mkubwa walioutoa na wanaoendelea kuutoa katika kuwezesha utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini.

Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani alitoa shukrani hizo jijini Dar es Salaam, Agosti 27, 2020 wakati wa kikao baina yake na Balozi wa Ufaransa hapa nchini, Frederic Clavier pamoja na Bjorn Midthun, ambaye ni Afisa Mwandamizi kutoka Ubalozi wa Norway nchini Tanzania.

“Mmefanya kazi nzuri sana katika kutuwezesha kutekeleza miradi ya umeme vijijini. Ushirikiano wenu umetuwezesha kufikia hatua hii tuliyopo leo. Kwa niaba ya Serikali, ninawashukuru sana,” alisisitiza Waziri.

Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Frederic Clavier (kushoto) na Bjorn Midthun, ambaye ni Afisa Mwandamizi kutoka Ubalozi wa Norway hapa nchini. Waziri alifanya kikao na Ujumbe husika, Agosti 27, 2020 Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, kujadili masuala ya ushirikiano katika sekta ya nishati.

Aidha, aliueleza Ujumbe huo kutoka Ufaransa na Norway kuwa vitongoji takribani 25,000 vimekwishafikishiwa umeme kati ya 64,339 vilivyopo nchini hivyo ameziomba nchi hizo kuendelea kutoa mchango wao katika kuwezesha kutekeleza kazi iliyobaki ya kupeleka umeme kwa vijiji na vitongoji vilivyosalia nchini.

Amesema umeme ni injini ya uchumi huku akipambanua kuwa pasipo umeme wa uhakika, haiwezekani kwa nchi yoyote kuwa na maendeleo ya kiuchumi.

Aliongeza kuwa jitihada za makusudi zinazoendelea kufanywa na Serikali hususani katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme, pamoja na mambo mengine, ndizo zimeiwezesha Tanzania, kuingia katika uchumi wa kati.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika kikao hicho, Balozi Clavier pamoja na Bwana Midthun, walimhakikishia Waziri Kalemani kuwa Serikali za nchi zao zitaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuwezesha miradi mbalimbali ya umeme.

Pamoja na kueleza utayari wa kuendelea kuisaidia Tanzania, Viongozi hao walisisitiza umuhimu wa kuzingatia viwango vya ubora katika kutekeleza miradi husika ambapo Waziri Kalemani amewahakikishia kuwa, ubora na uaminifu ni masuala yanayopewa umuhimu wa hali ya juu.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Mwakilishi wa Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Styden Rwebangira, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Amos Maganga na baadhi ya Maafisa Waandamizi kutoka REA, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Balozi za Norway na Ufaransa hapa nchini.