April 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yasema kufungiana mipaka kunaweka vikwazo katika biashara

Na Esther Macha,Times majira,Online, Mbeya

NAIBU Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kigahe amesema kuwa katika mikoa inayopakana na nchi za jirani kumekuwa  na mazingira ya kuwepo na changamoto ya nchi za Afrika za kufungiana mipaka na kuwekeana vikwazo visivyokuwa  vya msingi  katika kufanya biashara .

Amesema kuwa ipo haja ya nchi hizo kusaidiwa kufanya biashara bila vikwazo   na kwamba  kuna wakati inakuwa rahisi kufanya biashara na nchi za Ulaya na  bara la Asia kuliko kufanya biashara  kati ya  waafrika wenyewe.

Mh.Kigahe amesema hayo jana wakati wa ufunguzi wa kikao cha kamati ya ulinzi na usalama ambacho kimeshirikisha mikoa nane (8)ambayo ni Mbeya, Iringa, Njombe, Katavi ,Ruvuma,Rukwa, songwe  pamoja na Mkoa wa Tabora ambao unashirikiana na mikoa hiyo katika masuala ya  kulinda Uhifadhi.

“Na nyinyi mshajua sasa tumeingia mkataba kwenye eneo huru la biashara  Afrika maana yake ni lazima tuhakikishe tunapunguza vikwazo  ambavyo vinapelekea waafrika kutofanya biashara vizuri , kufungiana mipaka na kuwekeana vikwazo ambavyo havina umuhimu ambavyo vinarudisha nyuma  katika maendeleo na majirani zetu  na tunategemea sisi tuwe wa kwanza kupunguza vikwanzo hivi  namna yeyote ya kutofanya vizuri na wenzetu majirani , akitolea mfano nchi hizo kuwa ni Zambia,Zimbabwe, Congo, Malawi , Msumbiji , Afrika kusini  na kwingineko wanategemea sana lango la Tunduma hivyo lazima kufanya mazingira wezeshi  badala ya kuwekana vikwazo visivyo  na tija na nchi za wenzetu“amesema Naibu waziri .

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ,Juma Homera amesema kuwa lengo la kikao hicho ni kuangalia  masuala ya usalama nchi za wenzao, changamoto ya chakula  na usalama wa mipaka katika mikoa ya nyanda za juu kusini  pamoja Mkoa wa Tabora na kusema kwamba sababu za kuwepo mikoa huo katika kikao hicho ni kutokana na kushirikiana katika masuala ya ya kulinda uhifadhi.

Homera amesema kwamba kikao hicho ni kikao kazi ambacho huwa kinafanyika kwa mwaka mara mbili ambacho kinashirikisha wajumbe wote wa kamati zote za ulinzi na usalama mikoa yote ya Nyanda za juu kusini .

Kwa upande wake Kamshina msaidizi wa bajeti ya serikali anayesimamia mikoa na Halmashauri zote nchini  ,Andambike Mololo ambaye alimwakilisha Waziri wa Fedha  na mipango na kusema jukumu kubwa ola wizara ya fedha ni kusimamia na kubuni mipango ya fedha pamoja  na kuandaa bajeti ya nchi na kutimiza shughuli zote za uzalishaji wa nchi.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya ,Dkt.  Angelina Lutambi amesema kwamba kikao hicho ni cha ujirani mwema cha kamati za usalama za Mikoa lengo likiwa ni kujadili usalama na nchi za wenzao ,pamoja na usalama wa mipaka katika mikoa ya Nyanda za juu kusini.